Maguli kuiongoza Nakambala leo dhidi ya Zesco

Muktasari:

Ni siku ya Elias Maguli kudhihirisha uwezo wake ndani ya timu yake mpya ya Nakambala Leopard ya Zambia leo itakapocheza dhidi ya Zesco na anaanza kwenye kikosi cha kwanza.

Dar es Salaam.Mshambuliaji Mtanzania Elias Maguli leo ataichezea kwa mara ya kwanza timu yake ya Nakambala Leopard dhidi ya Zesco katika Ligi Kuu Zambia.

Maguli amejiunga na Nkambala Leopard akitokea KMC aliyovunja nayo mkataba kutokana na kutoelewana na viongozi.

Maguli alisema Ligi Kuu ya Zambia ilianza mwezi uliopita, alishindwa kuanza nao kwa sababu alikuwa anafuatilia vibali vya kumruhusu kuanza kazi nchini humo.

"Naanza kucheza leo dhidi ya Zesco, hii ni mechi muhimu kwangu kwani mashabiki wana hamu ya kuniona ni mchezaji wa aina gani baada ya kusikia nimesajiliwa."

"Ligi ya huku ina ushindani mkubwa, licha ya kwamba sikuanza kucheza mechi ya kwanza, nilikuwa naangalia mechi zilivyo tafu na namna ambavyo wachezaji wanapambana kuonyesha walichonacho."

"Ushindani unaanzia kwenye mazoezi, wanavyofanya utadhani kuna timu mbili pinzani, naamini nitakuwa na vitu vya tofauti vitakavyofanya nirejee kwenye kikosi cha Taifa Stars," alisema Maguli.