Pazi: Manula asipojiongeza atapotezwa Simba, Stars

Muktasari:

Hivi karibuni kocha Etienne Ndayyiragije wa Stars alimtumia Kaseja katika mechi zote mbili za kufuzu Chan dhidi ya Kenya ‘Harambee Stars’ ilielezwa Manula ni mgonjwa.

Dar es Salaam.Kipa namba moja wa Simba, Aishi Manula ameambiwa ajiongeze kama anahitaji kuendelea kuwa bora na chaguo la kwanza katika timu ya Taifa (Taifa Stars) na klabu yake ya Simba.

Kauli hiyo imetolewa na kipa mkongwe, Idd Pazi amesema Manula hivi sasa ana changamoto mbili katika kugombea namba katika timu ya Taifa na Simba.

"Inabidi ajiongeze, aweke msimamo na mkazo katika mazoezi yake binafsi mbali na yale ya timu ili aendelee kuwa bora.

"Amekutana na kigingi cha Juma Kaseja pale Stars, Kaseja ni kipa ambaye anafanya mazoezi sana na anapenda mazoezi binafsi, hivyo Manula akizembea kuongeza kasi ya mazoezi Kaseja anaweza kumuondoa kwenye kikosi cha kwanza timu ya Taifa.

Alisema kwenye klabu ya Simba pia kipa huyo ana changamoto ya namba na Beno Kakolanya ambaye amejiunga na timu hiyo msimu huu kwenye usajili wa dirisha kubwa baada ya kushindwana na Yanga.

"Beno pia ni kipa mzuri mwenye sifa zote za kuwa kipa, naye atahitaji kupambana ili kupata namba kwenye kikosi cha kwanza, hivyo atampa presha Manula ambaye inabidi apambane kweli kweli kuhakikisha anacheza kwa kiwango bora kila siku ili kuendelea kulinda nafasi yake Simba na hata Stars.