Kenya kutumia Jezi nyekundu dhidi ya Algeria leo

Muktasari:

Historia inaonesha kuwa kila wanapovaa jezi nyekundu, Kenya, iliyopangwa katika kundi C, pamoja na Algeria, Senegal na Tanzania, imekuwa ikipata matokeo chanya

Cairo, Misri. Mbivu na mbichi itajulikana pale Timu ya taifa ya Kenya, Harambee Stars, itakaposhuka katika Uwanja wa Jeshi wa Cairo, kuanza kampeni yao kwenye makala ya mwaka huu ya kombe la mataifa ya Afrika, (AFCON 2019), dhidi ya Algeria.

Mtanange huu utapigwa kuanzia saa tano usiku, muda mfupi baada ya majirani zao Tanzania, kupimana ubavu na Simba wa milima ya Teranga, Senegal, katika mchezo wa kwanza wa kundi C, utakaopigwa kuanzia saa mbili Usiku, kwenye uwanja huo huo wa Jeshi.

Kuelekea mechi yake na Algeria, imabainika kwamba Kenya, imepanga kutumia Jezi zao za Bahati dhidi ya kina Riyad Mahrez.  Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwenye kikao cha 'Pre-match', ni kwamba tofauti ilivyotarajiwa kuwa wangetumia jezi nyeupe, vijana wa Sebastien Migne, watatinga Macron Nyekundu.

Historia inaonesha kuwa kila wanapovaa jezi nyekundu, Kenya, iliyopangwa katika kundi C, pamoja na Algeria, Senegal na Tanzania, imekuwa ikipata matokeo chanya, kitu kilichowasukuma kutumia rangi hiyo kwenye mechi yao ya ufunguzi.

AFRIKA MASHARIKI

Fainali za mwaka huu, zimehuhudia ukanda wa Afrika Mashariki ikiweka rekodi ya kuingiza timu nne kwenye fainali hizi, katika historia ya soka lake, baada ya Burundi, Kenya, Tanzania na Uganda kufuzu, ambapo jana Juni 22, Uganda Cranes ilitutoa kimasomaso kwa kuitandika DR Congo 2-0, kabla Burundi wanaoshiriki kwa mara ya kwanza, kufa kiume dhidi ya Nigeria.