Kisa Real Madrid: Pogba kulazimisha kuondoka Manchester United

Muktasari:

Pogba anatarajiwa kusafiri kwa kwenda Marekani kupumzika wakati huo wakala wake, Mino Raiola akijaribu kufanikisha dili la mteja wake kujiunga na Real Madrid kwa kiwango kinachotajwa kuwa Paundi 150milioni.

London, England. Kiungo wa Manchester United, Paul Pogba yupo tayari kulazimisha uhamisho wa kuondoka Old Trafford na kumkia Hispania kujiunga na Real Madrid.

Mfaransa huyo ni miongoni mwa wachezaji walio katika rada za Real Madrid ambao wamempa fungu nono kocha wa kikosi hicho, Zinedine Zidane kwaajili ya kurejesha heshima yao msimu ujao.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka Hispania (ABC), zinaeleza kuwa Pogba yupo tayari kuchukua hatua zaidi ili kufanikisha uhamisho wa kujiunga na Real Madrid kipindi hiki cha usajili.

Kuna ripoti kuwa kiungo huyo wa zamani wa Juventus anaweza kukataa kujiunga na wachezaji wenzake mwezi ujao kuanza maandalizi ya msimu mpya wa 2019/20.

Pogba anatarajiwa kusafiri kwa kwenda Marekani kupumzika wakati huo wakala wake, Mino Raiola akijaribu kufanikisha dili la mteja wake kujiunga na Real Madrid kwa kiwango kinachotajwa kuwa Paundi 150milioni.

Tangu kiungo huyo arejee Manchester United akitokea Juventus kwa rekodi ya dunia ya Paundi 89 milioni wakati wa kiangazi 2016, Pogba ameshindwa kuonyesha thamani yake Old Trafford.

Kiungo huyo, hakuwa katika kiwango kiwango kizuri chini ya kocha aliyepita kwenye kikosi cha Manchester United, Jose Mourinho, uwepo wa   Ole Gunnar Solskjaer, kulimfanya kuanza kurejea katika kiwango chake.