Bondia Mwangata kuagwa kesho Dar, kuzikwa Mtwara

Muktasari:

Mwangata amewaibua na kuwaendeleza mabondia mbalimbali akiwano aliyekuwa nahodha wa timu ya Taifa ya ngumi, Joseph Martin na bondia Emmilian Patrick aliyefuzu kushiriki Olimpiki 2008.

Dar es Salaam.Mwili wa bondia bingwa wa zamani wa Afrika na kocha wa timu ya Taifa ya Ngumi za Ridhaa, Benjamin Mwangata utaagwa keshokutwa Jumatano mchana na kusafirishwa kwenda Mtwara kwa mazishi.

Mwangata alikutwa amefariki Jana Asubuhi nyumba kwake baada ya majirani kubomoa mlango.

Kaka wa Marehemu, Magnus Mwangata alisema keshokutwa Jumatano mwili wa Mwangata utachukuliwa hospitali ya Taifa Muhimbili kwenda nyumbani kwake Gongo la Mboto Ulongoni A ambapo utaagwa kabla ya kuelekea Mtwara kwa mazishi.

Mwangata  ameacha mke na watoto watatu mmoja akiwa bondia wa timu ya JKT ana rekodi ya kutwaa medali ya fedha ya michezo ya Afrika mwaka 1987 nchini Kenya.

Pia amewai kuiwakilisha nchi kwenye michezo ya Jumuiya ya madola ya 1990 na Olimpiki ya 1988 kabla ya kustaafu na kuwa kocha wa timu ya Taifa ya ngumi na klabu ya ngumi ya JKT.