Jento: Muziki wa dansi unaendeshwa kienyeji

Muktasari:

Jento amefanya kazi na bendi ya Beta Musica kabla ya kuanzisha The Dream Team FM Academia na baadaye akishirikiana na mwanamuziki Ndanda Kosovo wakaanzisha bendi ya Stono Musica 'wajelajela

Dar es Salaam. Mwalimu wa muziki THT, Kardinal Jento amesema ili kurudisha muziki katika hali yake ya zamani inabidi kuwepo na wawekezaji na wanamuziki wa dansi wawe na wasimamizi.

Jento aliyechangia kukuza vipaji vya wanamuziki Ben Pol, Amini, Linah, Rachel, Maunda Zorro, Mwasiti, Rubby, Nandy, Barnaba, Jay Melody, Benson, Mataluma, Vumilia, Ali Nipishe, Ditto, the Mafik.

Jento amesema muziki wa dansi unaendeshwa kienyeji na ukizingatia hali ya kiuchumi unakuta mwanamuziki washindwa kutengeneza video bora.

"Muziki wa dansi sasa hivi unaendeshwa kienyeji tu, huwezi kuwa unafanya muziki huku tunajipeleka wenyewe studio kwa hela yetu wenyewe  unatengeneza video kwa hela yako mwenyewe na hali ya uchumi yenyewe ni ngumu sana, tofauti na unavyoona kina Fally Ipupa, Ferre Gola wale wanakuwa na watu wanasimamia hivyo vitu wanakuwa na wawekezaji

"Hakuna biashara unayoweza kufanya bila mwekezaji, hapa Tanzania hakuna Lebo, mfano angalia wasafi, pale sio wote ni wakali kwenye muziki, hapana ila wapo tu kwenye usimamizi mzuri mtu anajua kazi yake kwenda kurekodi kuja kutoa ngoma nzuri, lakini sisi hapa wanamuziki wa dansi, unakuta unaingia studio na kutengeneza video kwa hela yako mwenyewe unatoa kazi."

Jento amewahi kutamba na kibao chake cha Mundende, Kula kuku kula mayai na Dhahabu, alianza kuwa mwalimu wa THT toka mwaka 2005 hadi sasa, na kabla hajajiunga na chuo hiko alipofika Tanzania mwaka 1994 alikiunga na bendi ya Beta Musica kabla ya kuanzisha The Dream Team FM Academia na baadaye akishirikiana na mwanamuziki Ndanda Kosovo wakaanzisha bendi ya Stono Musica 'wajelajela.