Masikini Bale ashindwa kuaga Real Madrid

Madrid, Hispania. Real Madrid imemaliza msimu vibaya kwa kichapo cha mabao 2-0 kwenye uwanja wake dhidi ya Real Betis.

Pamoja na kufungwa, mshambuliaji Gareth Bale hakupata fursa ya kuaga mashabiki wa klabu hiyo kwa kuwa msimu ujao hatakuwapo Santiago Bernabeu.

Bale alikuwapo kwenye benchi, lakini hakucheza wala kufanya mazoezi mepesi ya kuingia katika mchezo huo ambao Real Madrid ilikuwa nyumbani kwenye Uwanja wa Santiago Bernabeu.

Nyota huyo aliyekuwa amevaa suti ya michezo ya rangi ya bluu, alionekana akiteta jambo na mmoja wa maofisa kabla ya kuingia ndani ya vyumba vya kuvalia nguo, baada ya mchezo kumalizika.

Bale hakupata muda wa kuwapungia mkono wa kuwaaga mashabiki kama wanavyofanya mastaa mbalimbali wanapomaliza muda wao ndani ya klabu.

Mabao ya Loren Moron na Jese yalitosha kumaliza vibaya siku ya kocha Zinedine Zidane.