Lacazette anatoka Lemar anaingia

LONDON ENGLAND. DILI sio dili? Arsenal wameripotiwa wanaweza kumruhusu Alexandre Lacazette kwenda Atletico Madrid huku Thomas Lemar akitua Emirates.

Baada ya janga la corona kusababisha matatizo makubwa ya kiuchumi kwa klabu jambo ambalo limeathiri soko la wachezaji wakati dirisha la uhamisho litakapofunguliwa hivi karibuni.

Kutokana na hilo dili nyingi za timu katika maandalizi ya msimu mpya wa 2020-21 zinaweza kuwa za kubadilishana wachezaji baada ya pesa kuwa magumu.

Arsenal ilihusishwa na mpango wa kumsajili Lemar kwenye dirisha la Januari, mwaka huu na sasa imedaiwa ina mpango wa kubadilishana Wafaransa huyo.

Lemar, ameshindwa kufunga wala kuasisti katika mechi 24 alizocheza akiwa Atletico Madrid chini ya Diego Simeone, lakini alikuwa kwenye kiwango bora sana wakati akiwa AS Monaco kabla ya kutimkia Hispania.

Lacazette, wakati huo huo, anaripotiwa anaonekana atakwenda kuwa wa ziada katika kikosi cha Arteta akija na mipango yake moto ya kufanya mabadiliko kwa washambuliaji wake.

Kwa mujibu wa Fichajes, Arsenal inapanga kutumia Lacazette kama chambo ili wampate Lemar, ambaye kwa siku za karibuni amekuwa akihusishwa pia na dili la uhamisho wa kwenda Manchester United pale Old Trafford.