Iker Casillas mkewe wote majanga tupu

Muktasari:

Casillas ametangaza kustaafu soka baada ya kucheza kwa zaidi ya miaka 20, alipoingia katika kikosi cha kwanza cha Real Madrid mwaka 1999.

Madrid, Hispania. Mke wa staa wa Kihispaniola, Iker Casillas mrembo Sara Carbonero amefichua kuwa na tatizo la kansa ya kizazi ikiwa ni wiki chache tu zimepita tangu mumewe alipopata shambulio la moyo akiwa mazoezini FC Porto.

Mrembo Sara Carbonero alifichua jambo hilo kupitia ujumbe wake aliotuma kwenye mtandao ya kijamii, akiandika: “Tukiwa bado hatujaondoka kwenye ule mshtuko wa mwanzo, maisha yametuletea majaribu mengi.

“Safari hii ni mimi, neno lenye hefuri sita linanipa shida kuliandika. Siku chache zilizopita baada ya kufanya vipimo vya afya, daktari alisema kuna shida kwenye mirija yangu ya uzazi, hivyo nikafanya upasuaji. Nina kansa ya kizazi. Naamini kila kitu kitakwenda sawa, lakini ndiyo hivyo inahitaji mapambano makubwa. Nashukuru kwa sapoti ya familia yangu, mashabiki na madaktari.”

Mrembo huyo ambaye ni mtangazaji wa televisheni alimnasa Casillas kupitia kazi yake hiyo hasa kwenye fainali za Kombe la Dunia 2010 zilizofanyika Afrika Kusini ambapo Hispania ya kipa Casillas ndiyo iliyobeba ubingwa.

Sara amefanikiwa kupata watoto wawili wa kiume aliozaa na mumewe huyo kipa maarufu kabisa kwenye soka la Hispania na katika klabu ya Real Madrid kabla ya kutimkia Porto.