VIDEO- Maelfu wajitokeza kumpokea Maradona akitambulishwa kuwa kocha

Muktasari:

Nyota huyo wa zamani wa Argentina atakuwa na kazi ya kuifundisha klabu ya Gimnasia ambayo iko mkiani mwa Ligi Daraja la Kwanza.


Shangwe za furaha zilikuwa ni lazima wakati wa mashabiki wa klabu ya Gimnasia ya La Plata walipojitokeza kwa maelfu kumlaki gwiji wa soka duniani, Diego Maradona kuwa kocha mpya wa klabu hiyo.


Takriban mashabiki 30,000 walijitokeza kwenye Uwanja wa Del Bosque katika sherehe ya kumtambulisha nyota huyo wa zamani wa timu ya taifa ya Argentina na klabu ya Napoli.


Gwiji huyo anayejulikana kama Golden Boy kwa mashabiki wa soka wa Argentina aliteuliwa kuwa kocha wa klabu hiyo kongwe wiki iliyopita.


Umaarufu wa klabu hiyo unatokana na enzi zake ilipotwaa ubingwa wa ligi daraja la pili mara tatu (1944, 1947 na 1952), ikiwa ni pamoja na kutwaa ubingwa wa Centenary Cup, michuano iliyoandaliwa kuadhimisha miaka 100 tangu kuanzishwa ligi daraja la kwanza Argentina.


Hivi sasa klabu hiyo iko mkiani wa ligi daraja la kwanza, Primera Division.


Na maradona, ambaye aliacha kazi ya ukoicha wa timu ya taifa ya Argentina miaka tisa iliyopita, atakuwa na kazi ya kuhakikisha Gimnasioa inabaki Ligi Daraja la Kwanza.


Kwenye mkutano na waandishi wa habari baada ya mazoezi yake ya kwanza, Maradona alionekana kuwa mtu mwenye hisia.