Vita ya ubingwa EPL iko hapa
Muktasari:
- Dan Ballard aliitanguliza Sunderland kwa bao la kwanza, lakini Arsenal ilijibu mapigo ikifunga mara mbili kupitia kwa Bukayo Saka na Leandro Trossard, kabla ya Brobbey kufunga kwenye dakika za mwisho kabisa kufanya mechi hiyo kumalizika kwa sare ya mabao 2-2.
LONDON, ENGLAND: MAMBO yamezidi kunoga. Matumaini ya Arsenal yalikuwa ni kuondoka kwenye mechi ya ugenini dhidi ya Sunderland kwa kuzoa pointi zote tatu baada ya kupindua meza, lakini Brian Brobbey, alikuja kutibua mambo dakika za mwisho kabisa Stadium of Light.
Dan Ballard aliitanguliza Sunderland kwa bao la kwanza, lakini Arsenal ilijibu mapigo ikifunga mara mbili kupitia kwa Bukayo Saka na Leandro Trossard, kabla ya Brobbey kufunga kwenye dakika za mwisho kabisa kufanya mechi hiyo kumalizika kwa sare ya mabao 2-2.
Licha ya Arsenal kwenda kwenye mechi hiyo ikiwa na rekodi matata kabisa ya kucheza mechi nane za michuano yote bila ya kuruhusu bao, lakini staa wa Sunderland, Ballard alitibua rekodi hiyo baada ya kumchambua kipa David Raya kufuatia pasi ya kichwa ya Nordi Mukiele na kumtikisa kiungo wa The Gunners, Declan Rice.
Dakika tisa baada ya kuanza kipindi cha pili, Bukayo Saka aliisawazishia Arsenal. Kisha Leandro Trossard aliongeza bao jingine kali kwa Arsenal na kuifanya kuongoza 2-1 katika dakika 15 za mwisho.
Hata hivyo, mambo hayakuishia hapo, mtokea benchini Brobbey alifunga katika dakika za jiooni kabisa kuifanya Sunderland kupata pointi moja kwenye uwanja wake wa nyumbani.
Sare hiyo iliamsha ahueni kwa timu za Manchester City na Liverpool, ambazo zitamenyana zenyewe leo Jumapili uwanjani Etihad, ikiwa ni mchakamchaka wa kuwania ubingwa wa ligi.
Baada ya raundi hiyo ya 11 kwenye Ligi Kuu England, mjadala ni mechi tano zijazo kwa kila timu za Arsenal, Man City na Liverpool kwenye vita ya kusaka ubingwa wa taji hilo.
1. Arsenal - mechi 11, pointi 26
Arsenal ipo kileleni kwenye msimamo wa ligi, lakini mechi zao tano zijazo watakuwa na kasheshe la kukabiliana na mechi kadhaa za ugenini ambazo ni ngumu kwelikweli.
Baada ya mechi za kimataifa, Arsenal itakabiliana na mahasimu wao Tottenham. Kisha itakuwa na mechi nyingine ngumu ya London huko Stamford Bridge kukabiliana na Chelsea.
Baada ya hapo itakipiga na Brentford kabla ya kukabiliana na Aston Villa na kumalizia na Wolves.
2. Liverpool - mechi 10, pointi 18
Kabla ya mechi ya Jumapili dhidi ya Man City, Liverpool ilikuwa imevuna pointi 18 katika mechi 10. Mechi hiyo ilikuwa ugenini uwanjani Etihad na baada ya hapo, itarudi Anfield kucheza na Nottingham Forest.
Baada ya hapo, itakuwa na kipute cha ugenini kukabiliana na West Ham, kisha itarudi nyumbani kucheza na Sunderland na baadaye ugenini dhidi ya Leeds United. Mchezo wa tano wa ligi ukiweka kando wa Man City, Liverpool itakuwa Anfield kucheza na Brighton.
3. Man City - mechi 10, pointi 19
Man City ilikuwa nyumbani kucheza mechi yake ya 11 kwenye Ligi Kuu England msimu ilipokabiliana na Liverpool uwanjani Etihad, Jumapili.
Baada ya mechi hiyo, ratiba yake ya mechi tano zijazo inawapa mwanga wa kufahamu hatima ya vita yao kwenye mbio za ubingwa wa Ligi Kuu England msimu huu.
Man City itaanzia ugenini kumenyana na Newcastle, kisha itarudi nyumbani kucheza na Leeds United, kisha itaenda ugenini kucheza na Fulham na baadaye Etihad kucheza na Sunderland na kumaliza mchezo wake wa tano kwa kukabiliana na Crystal Palace uwanjani Selhurst Park.