Utani wamponza staa Chelsea
Muktasari:
- Mshambuliaji huyo hakuwa katika kikosi cha Chelsea kilichocheza dhidi ya Liverpool jana Jumamosi, Oktoba 04 na kuibuka na ushindi wa mabao 2-1.
LONDON, ENGLAND: MASHABIKI wa Chelsea walikasirishwa sana na kitendo cha mchezaji wao Jorrel Hato kuonekana akimfanyia utani kwa kumrukia staa wao mwingine Cole Palmer ambaye kwa sasa yupo nje kutokana na majeraha.
Mshambuliaji huyo hakuwa katika kikosi cha Chelsea kilichocheza dhidi ya Liverpool jana Jumamosi, Oktoba 04 na kuibuka na ushindi wa mabao 2-1.
Palmer, mwenye umri wa miaka 23, alilazimika kutoka kiwanjani kwenye mechi dhidi ya Manchester United Septemba mwaka huu kutokana na jeraha la nyonga.
Baada ya vipimo madaktari wamesema atatakiwa kuwa nje kwa wiki tatu hadi nne, hivyo akawa mmoja kati ya wachezaji wanane wa Chelsea waliokosa mechi hiyo kutokana na majeraha na adhabu.
Katika mechi hiyo dhidi ya Liverpool, Chelsea ilipata pigo jingine baada ya Benoit Badiashile na Josh Acheampong kulazimika kutoka uwanjani kutokana na majeraha.
Mastaa hawa wanaungana na wachezaji wenzao wengine kama Levi Colwill, Dario Essugo, Tosin Adarabioyo, Andrey Santos na Liam Delap ambao wamekuwa nje kwa majeraha ya muda mrefu.
Mashabiki walichukizwa na kitendo cha Hato alichokifanya dakika chache baada ya kumalizika kwa mechi ya Liverpool.
Tukio hilo lilitokea wakati wachezaji wakiwa wanashangilia ushindi walioupata na Hato, mwenye umri wa miaka 19, alionekana akimrukia Palmer ambaye baada ya hapo alionekana kukunja uso kama ishara ya kupata maumivu kisha akaweka mikono yake katika kiuno ishara ya kushika eneo ambalo lina maumivu yanayosababisha akae nje hadi sasa.
Mashabiki walipatwa na wasiwasi kutokana na hali hiyo na kupiti mitandao ya kijamii mmoja aliandika: “Hali yake haionekani kuwa ni nzuri kabisa,” mwengine akaandika, “Hato anafanya nini?”, “Anamwongezea maumivu tu, naona anamfanya akae nje kwa mwezi mwingine mmoja.”
Akizungumza kabla ya ushindi, kocha Enzo Maresca alisisitiza kuwa hakuna taarifa mpya kuhusu ni lini Palmer atarejea ingawa alionekana kuwa na matumaini kwamba atarudi baada ya mapumziko ya kimataifa.
Amesema: “Sina taarifa yoyote kwa sasa kuhusu Palmer. Tuna mkutano wiki hii kuona hali yake na kisha tutaamua ikiwa anaweza kurudi baada ya mapumziko ya kimataifa.”
Palmer atakosa mechi ya kirafiki dhidi ya England dhidi ya Wales itakayopigwa kwenye dimba la Wembley Alhamisi ya wiki hii, pamoja mechi ya kufuzu Kombe la Dunia ugenini dhidi ya Latvia itakayochezwa kwenye Uwanja wa Daugava, Riga, Oktoba 14.
Vilevile huenda akakosa mechi ijayo ya Chelsea itakayokuwa ya ugenini Oktoba 18, kwenye Uwanja wa City Ground dhidi ya Nottingham Forest.