Siri imevuja! Sakata la Alonso laipasua Real Madrid, wachezaji wavutana
Muktasari:
- Mgogoro huo umefafanuliwa tukio hilo ni kama vita vya ndani, hali inayotishia utulivu wa timu hiyo inayoongoza msimamo wa Ligi Kuu Hispania 'La Liga'.
Klabu ya Real Madrid inadaiwa kukumbwa na mgawanyiko mkubwa ndani ya chumba cha kubadilishia, huku taarifa zikidai kuna kundi la wachezaji ambao hawamtaki kocha Xabi Alonso aendelee, na wengine wanaomuunga mkono kikamilifu.
Mgogoro huo umefafanuliwa tukio hilo ni kama vita vya ndani, hali inayotishia utulivu wa timu hiyo inayoongoza msimamo wa Ligi Kuu Hispania 'La Liga'.
Kwa mujibu Daily Mail, baadhi ya wachezaji wakubwa wanahisi kuwa mbinu na uamuzi wa Xabi Alonso hauwafaidishi, wakilalamikia mfumo wa uchezaji na jinsi anavyotumia baadhi ya wachezaji muhimu.
Kundi hilo linadaiwa kuamini kuwa mabadiliko ya benchi la ufundi yanaweza kuirudisha timu kwenye ubora uliotarajiwa, na sio kuendelea na Alonso aliyechukua nafasi ya Carlo Ancelotti mwishoni mwa msimu uliopita.
Hata hivyo, kuna kundi lingine la wachezaji ambao wapo nyuma ya kocha huyo raia wa Hispania, wakiona Alonso anajaribu kujenga mpango wa muda mrefu na kuleta nidhamu ambayo inajenga mwelekeo mpya ndani ya kikosi cha Real Madrid.
Kundi hilo linadai kuwa, shinikizo la kumng’oa kocha Alonso halitasaidia mabadiliko ndani ya Real Madrid, bali litazidisha migogoro ambayo itawarudisha nyuma.
Hali hiyo ya mvutano imeifanya klabu kuingia kwenye kipindi kigumu, huku mashabiki na viongozi wakifuatilia kwa karibu kuona ni upande gani utapata nguvu zaidi kwenye mustakabali wa Xabi Alonso klabuni hapo.