Saka ndiye tajiri wao mpya Arsenal
Muktasari:
- Winga huyo ataendelea kubaki Arsenal baada ya kuingia katika miezi 18 ya mwisho ya mkataba wake wa awali mwanzoni mwa mwaka mpya.
LONDON, ENGLAND: MISHAHARA inayolipwa kwenye kikosi cha Arsenal imewekwa bayana baada ya supastaa Bukayo Saka kukubali kusaini mkataba mpya wa miaka mitano.
Winga huyo ataendelea kubaki Arsenal baada ya kuingia katika miezi 18 ya mwisho ya mkataba wake wa awali mwanzoni mwa mwaka mpya.
Inaripotiwa kuwa Saka amekubali kuongeza mkataba wake hadi 2031, jambo ambalo ni ushindi mkubwa kwa kocha Mikel Arteta.
Sasa Saka atakuwa akipokea mshahara wa kushangaza wa Pauni 300,000 kwa wiki katika Uwanja wa Emirates.
Hii inamfanya Saka kuwa mchezaji anayelipwa zaidi kaskazini mwa London huku timu yake ikiendelea kusukuma kuelekea ubingwa.
Arsenal imetumia fedha nyingi katika harakati zao za kutwaa mataji makubwa. Na bili yao ya mishahara inaonyesha wazi kuwa Arteta hana mipaka katika juhudi zake za kuandika historia.
Kwa kuwa Saka ndiye anayelipwa zaidi, kuna wachezaji wasiopungua sita wengine wanaopokea Pauni 200,000 au zaidi kwa wiki. Kai Havertz ndiye wa pili kwa mshahara mkubwa akilipwa Pauni 275,000 kwa wiki, akifuatiwa na William Saliba Pauni 250,000 kwa wiki, Declan Rice Pauni 225,000 kwa wiki, Martin Odegaard na Gabriel Jesus, kila mmoja akilipwa Pauni 220,000 kwa wiki, huku straika Viktor Gyökeres akipokea Pauni 200,000 kwa wiki.
Cha kushangaza zaidi, wachezaji wengine 11 pia wanapokea mishahara ya tarakimu sita kila wiki. Gabriel Martinelli, Eberechi Eze, Gabriel Magalhaes na Ben White wote wapo katika kundi la juu la wanaolipwa vizuri. Jurrien Timber, Riccardo Calafiori na Mikel Merino nao pia wanapokea mishahara minono.
Vilevile, Piero Hincapié, Martin Zubimendi, Leandro Trossard na David Raya kila mmoja analipwa Pauni 100,000 kwa wiki.
Hata wachezaji wa akiba wa Arsenal wanalipwa vizuri, huku Christian Norgaard, Kepa Arrizabalaga na Christian Mosquera wakipata pesa nyingi licha ya kupata dakika chache uwanjani.
Hata hivyo, Noni Madueke anaonekana kulipwa chini ya kiwango chake, akipata Pauni 50,000 kwa wiki licha ya kuwa na mchango mkubwa msimu huu. Vijana chipukizi Ethan Nwaneri na Myles Lewis-Skelly wote wanapokea Pauni 40,000 kwa wiki.
Wakati huo huo, kijana Max Dowman bado yuko kwenye mkataba wa mwanafunzi unaomlipa kiasi kidogo cha Pauni 350 kwa wiki, hadi atakapofikisha miaka 17, Desemba mwaka huu.