Saka amerudi, Havertz, Ødegaard kuiwahi Atletico
Muktasari:
- Kwa sasa, macho yote yanaelekezwa kwenye pambano la marudiano, na Arsenal itahitaji kikosi chao kamili ili kupambana kusaka tiketi ya fainali.
LONDON, ENGLAND: KOCHA wa Arsenal, Mikel Arteta ametoa taarifa za majeruhi kuelekea mchezo wa marudiano wa nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Atletico Madrid, huku akiwapa matumaini mashabiki wake.
Nyota wa kikosi hicho, Bukayo Saka alirejea kikosini kwa kiwango kikubwa katika ushindi wa 3-0 dhidi ya Fulham na alifunga na kung’ara kabla ya kutolewa mapema kipindi cha pili.
Arteta alieleza mabadiliko hayo yalikuwa ya tahadhari kutokana na hali ya utimamu wa Saka.
“Alilazimika kutoka. Alicheza dakika kadhaa Madrid, sasa amecheza dakika 45. Tunahitaji kumwongeza taratibu lakini kwa umakini kwa sababu tunamhitaji uwanjani,” amesema Arteta.
Kocha huyo ameongeza hali ya Saka imeimarika zaidi.
“Maumivu yameisha, sasa yuko huru na ametulia. Huyu ndiye Saka tunayemhitaji na kiwango chake ni msingi mkubwa kuelekea mchezo wa Jumanne.”
Kwa upande mwingine, wachezaji Kai Havertz na Martin Ødegaard, ambao hawakucheza dhidi ya Fulham, wanatarajiwa kurejea kwa mechi hiyo muhimu.
“Nadhani watarejea. Watafanya kila wawezalo na sisi pia kuhakikisha wanakuwa tayari kwa mchezo huo,” ameongeza Arteta.
Hata hivyo, Arsenal itamkosa Mikel Merino ambaye hatacheza kabisa, huku Jurrien Timber akiwa na uwezekano mdogo wa kuwepo kutokana na kutokuwa fiti kwa sasa.
Kwa sasa, macho yote yanaelekezwa kwenye pambano la marudiano, na Arsenal itahitaji kikosi chao kamili ili kupambana kusaka tiketi ya fainali.