Ronaldo ampa jeuri kocha Juventus

TURIN, ITALIA. KOCHA wa Juventus, Andrea Pirlo ameonekana kuwa na matumaini makubwa  ya kuiongoza  timu hiyo  kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu Italia maarufu kama Serie A kwa kuahidi  kwamba watapambana hadi mwisho dhidi ya  Inter Milan na  AC Milan.

Usiku wa Jumatatu, Juventus  iliibuka na ushindi wa mabao 3-0  dhidi ya  Crotone. Aliyekuwa shujaa kwa upande wao kwenye mchezo huo alikuwa ni Cristiano Ronaldo aliyetupia mbili na kuisaidia timu hiyo kusogea hadi nafasi ya tatu.

Zimebaki pointi nane kwa Juventus wenye mchezo mmoja mkononi  kuifikia Inter Milan ambao ndio vinara wa Ligi Kuu Italia wakiwa na pointi 53.

""Tulianza kuwa na wasiwasi kidogo, labda baada ya kufungwa mchezo wetu wa mwisho hicho ndicho kitu kilichochangia kuwa na  wasiwasi, Lakini mabao tuliyofunga  yalitusaidia na kutupa utulivu wa akili," amesema kocha huyo.

Kwa sasa Inter Milan wanaonekana kutawala mbio za ubingwa wa Serie A  baada ya kuitwanga AC Milan siku chache zilizopita kwenye mchezo wa mahasimu 'Derby della Madonnina'.

"Ilikuwa mechi muhimu kwetu na  jambo muhimu ni kwamba tumepata pointi tatu huku cha  kuvuti hatukuruhusu bao," amesema kiungo wa timu hiyo,  Aaron Ramsey.