Dah! Pogba apata kimeo kingine
Muktasari:
- Pogba alikuwa na matumaini ya kucheza mechi yake ya kwanza baada ya mapumziko ya kupisha mechi za kimataifa, lakini sasa majeraha aliyopata yanamweka kwenye hatihati.
MONACO, UFARANSA: KIUNGO wa AS Monaco, Paul Pogba amepata pigo baada ya kuumia na sasa ataendelea kusubiri kabla ya kucheza mechi yake ya kwanza kwenye kikosi hicho cha miamba ya Ufaransa.
Pogba alikuwa na matumaini ya kucheza mechi yake ya kwanza baada ya mapumziko ya kupisha mechi za kimataifa, lakini sasa majeraha aliyopata yanamweka kwenye hatihati.
Kiungo huyo wa zamani wa Juventus na Manchester United anaripotiwa kuumia mazoezini na hivyo ataendelea kusubiri kabla ya kucheza mechi yake ya kwanza.
Mpango ulikuwa Pogba acheze mechi yake ya kwanza, Jumamosi ya Oktoba 18 dhidi ya Angers.
Staa huyo wa zamani wa Les Bleus hajacheza mechi yoyote ya kiushindani tangu Septemba 2023 kutokana na kukumbana na adhabu ya kufungiwa kufuatia kufeli kwenye vipimo vya matumizi ya dawa za kusisimua misuli, ambapo awali alifungiwa miaka minne ambayo ilipunguzwa na kuwa miezi tisa baada ya kukata rufaa.
Alijiunga na AS Monaco kwenye dirisha lililopita la uhamisho wa majira ya kiangazi.