Mali, Zambia hakuna mbabe, Daka akimtungua Diarra
Muktasari:
- Katika mechi hiyo, Mali ilitangulia kwa bao la Lassine Sinayoko katika dakika 61 na kuonekana kama mechi ingekuwa nzuri kwa upande wao kabla ya mabeki wa timu hiyo kuzembea kwenye kumdhibiti Daka, aliyepita katikati yao na kuunganisha kwa kichwa krosi ya Mathews Banda na hivyo mpira kumshinda kipa Djigui Diarra.
CASABLANCA, MOROCCO: BAO la dakika za majeruhi la Patson Daka limeiokoa Zambia kukumbana na kichapo mbele ya Mali baada ya kutoka sare ya 1-1 kwenye mechi ya kwanza ya Kundi A katika mashindano ya AFCON 2025 iliyofanyika kwenye Uwanja Stade Mohamed V jioni ya leo Jumatatu.
Katika mechi hiyo, Mali ilitangulia kwa bao la Lassine Sinayoko katika dakika 61 na kuonekana kama mechi ingekuwa nzuri kwa upande wao kabla ya mabeki wa timu hiyo kuzembea kwenye kumdhibiti Daka, aliyepita katikati yao na kuunganisha kwa kichwa krosi ya Mathews Banda na hivyo mpira kumshinda kipa Djigui Diarra.
Hata hivyo, Mali inapaswa kujilaumu yenyewe kwa kushindwa kuondoka uwanjani na pointi zote tatu baada ya kukosa penalti katika kipindi cha kwanza, wakati mkwaju wa El Bilal Toure ulipopanguliwa na kipa Willard Mwanza.
Matokeo hayo yanafanya Mali na Zambia kugawana pointi katika kundi hilo, linaloongozwa na vinara Morocco, ambao ndio wenyeji wa mashindano hayo baada ya kuichapa Comoro 2-0 katika mechi ya ufunguzi iliyofanyika Jumapili.
Kocha wa Mali, Tom Saintfiet sasa atalazimika kupanga vyema karata zake kwa ajili ya mechi ya pili katika kundi hilo ambapo atakabiliana na wenyeji Boxing Day (Desemba 26), wakati Zambia ya kocha Moses Sichone nayo itashuka uwanjani siku hiyo kukabiliana na Comoro, inayoburuza mkia kundini kutokana na kutokuwa na pointi yoyote baada ya kichapo kutoka kwa Simba wa Atlas.
MECHI ZIJAZO
ZA KUNDI A
Desemba 26, 2025
Zambia v Comoros (Saa 2:30 usiku)
Morocco v Mali (Saa 5:00 usiku)
Desemba 29, 2025
Comoros v Mali (Saa 4:00 usiku)
Zambia v Morocco (Saa 4:00 usiku)