Kwa hili la bosi wa Nottingham Forest, usijaribu kabisa
Muktasari:
- Wikiendi iliyopita, Marinakis alimfukuza Ange Postecolgu baada ya matokeo mabovu ya timu hiyo tangu achukue mikoba ya kuinoa.
NOTTINGHAM, ENGLAND: 'SHANGILIA lakini usiniguse', Ndivyo inavyoweza kusemwa ukiwa karibu na Mwenyekiti wa Nottingham Forest, Evangelos Marinakis kutokana na wiki ngumu ambayo amekuwa akipitia inayosababisha na matokeo ya timu zake anazozimiliki.
Wikiendi iliyopita, Marinakis alimfukuza Ange Postecolgu baada ya matokeo mabovu ya timu hiyo tangu achukue mikoba ya kuinoa.
Postecoglou, aliyeteuliwa mwezi uliopita kuchukua nafasi ya Nuno Espirito Santo aliyefukuzwa mwanzoni mwa msimu huu, amekaa siku 39 na kuiongoza Forest katika mechi nane pekee za michuano yote ambazo zote hakuambulia ushindi hata moja.
Siku moja tu baada ya kumtimua Postecoglou, timu nyingine inayomilikiwa na bilionea huyu, Rio Ave ya Ureno, ilitolewa kwenye Kombe la Ureno (Taca de Portugal) baada ya kupoteza kwa mabao 3-2 dhidi ya S.U. Sintrense, timu ya daraja la nne.
Kama ilivyo kwa Forest, Rio Ave pia imeanza msimu vibaya ikiwa imefanikiwa kushinda mchezo mmoja pekee kati ya nane ya mwanzo katika ligi kuu ya Ureno.
Wakati huo huo, klabu ya kwanza ambayo Marinakis aliwahi kuinunua mwaka 2010, Olympiacos ya Ugiriki, iliendelea kuongeza maumivu kwa tajiri huyo baada ya kuchapwa mabao 6-1 dhidi ya Barcelona kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya, katika mechi ambayo iligubikwa na utata baada ya mchezaji wao kutolewa nje kwa kadi nyekundu sekunde chache tu baada ya kufunga bao.
Wiki mbaya inaweza ikaendelea tena kwa bilionea huyo kutokana na matokeo yanayoweza kutokea kwa timu anazomiliki wikiendi hii na Rio Ave itashuka dimbani kuvaana na C.F. Estrela da Amadora katika Ligi Kuu Ureno, Forest itaumana na Bournemouth baada ya mechi ya Europa League wakati Olympiacos ikiumana na AEK Athens F.C, Oktoba 26.