Kocha Spurs aionya West Ham United
Muktasari:
- Katika mechi zijazo, Spurs itakuwa na safari ya kuifuata Aston Villa, kabla ya kukutana na Leeds United na Everton nyumbani, kisha itamaliza safari yake ya msimu huu ugenini dhidi ya Chelsea.
LONDON, ENGLAND: KOCHA wa Tottenham, Roberto De Zerbi ameionya West Ham United kuwa klabu yake ipo tayari kupambana kuhakikisha wanabaki Ligi Kuu England ikiwa ni baada ya kupata ushindi wao wa kwanza wa ligi wikiendi iliyopita, tangu kuanza kwa mwaka 2026.
Baada ya mechi dhidi ya Wolves iliyomalizika kwa Spurs kushinda bao 1-0, De Zerbi amesema: "Ninaamini tunaweza kubaki ligi kuu. Sio tofauti ya pointi 10, tuko pointi mbili tu nyuma ya West Ham, ambao ni timu nzuri, lakini sisi pia ni timu nzuri sana. Kitu muhimu ni ubora wa wachezaji wangu na namna wanavyojitoa. Nilipowafahamu vizuri, nilijua tuna nafasi ya kubaki. Ukiangalia mechi kwenye TV huwezi kuona roho yao ya kupambana, lakini mimi nafanya kazi nao kila siku, wote ni wachezaji wa maana na watu wazuri wanaopitia kipindi kigumu.”
Hata hivyo, De Zerbi hakuridhishwa kabisa na kiwango cha timu yake, akisema matokeo mabaya ya muda mrefu yaliathiri hali yao ya kujiamini:
"Dakika 35 za kwanza tulicheza vizuri, lakini hatukutengeneza nafasi nyingi. Kipindi cha pili sikukipenda kabisa tunapaswa kucheza vizuri zaidi."
Pia De Zerbi alieleza wasiwasi kuhusu majeraha ya Xavi Simons na Dominic Solanke, akisema: "Solanke ana tatizo la misuli, si kubwa sana, lakini sijui atakosa mechi ngapi. Kuhusu Xavi, goti huwa ni jambo nyeti tutajua zaidi Jumatatu au Jumanne. Sipendi kupoteza wachezaji zaidi. Tunaweza kushinda mechi, lakini lazima tuwe na wachezaji, si kwa makocha."
Kwa sasa Spurs imebakiwa na mechi nne, ikiwa pointi mbili nyuma ya West Ham.
Katika mechi zijazo, Spurs itakuwa na safari ya kuifuata Aston Villa, kabla ya kukutana na Leeds United na Everton nyumbani, kisha itamaliza safari yake ya msimu huu ugenini dhidi ya Chelsea.