Kocha Man United hataki kujiuzulu

Muktasari:
- Kocha huyo raia wa Ureno alithibitisha kuwa atalipa kwa gharama zake binafsi kuwapeleka wafanyakazi wake 30 na familia zao kushuhudia fainali ya Jumatano dhidi ya Tottenham huko Uhispania.
MANCHESTER, ENGLAND: KOCHA wa Manchester United, Ruben Amorim ameweka wazi kwamba hana nia ya kujiuzulu kuifundisha timu hiyo lakini anajua shinikizo litaongezeka ikiwa hatashinda Europa League.
Kocha huyo raia wa Ureno alithibitisha kuwa atalipa kwa gharama zake binafsi kuwapeleka wafanyakazi wake 30 na familia zao kushuhudia fainali ya Jumatano dhidi ya Tottenham huko Uhispania.
Amorim aliwashangaza mashabiki baada ya kipigo cha Jumapili dhidi ya West Ham alipokiri kuwa atalazimika kuondoka ikiwa hatabadili mwenendo wa Manchester United mwanzoni mwa msimu ujao.
Amorim, ambaye ameshinda mechi sita pekee kati ya 25 za Ligi Kuu akiwa kocha, alisema: “Tangu nilipowasili hapa nimekuwa nikizungumzia viwango. Siwezi kuona timu ikiwa na matokeo kama haya — hasa katika Ligi Kuu, halafu nisiwe na la kusema au kuwajibika.”
“Ni hayo tu. Nina wazo la nini cha kufanya. Ninaelewa matatizo ya timu na sipo karibu kujiuzulu.”
“Kile ninachosema ni kwamba tunapaswa kufanya vizuri msimu huu na katika siku za usoni la sivyo nitaondoka. Hilo ni jambo la kawaida kwa makocha wote. Ndivyo nilivyohisi baada ya West Ham na bado ndivyo ninavyohisi leo.”
Amorim anaamini kuwa ikiwa timu hiyo itapoteza dhidi ya Tottenham ambao hawajashinda taji lolote tangu 2008 kutazidisha shinikizo la kuondoka kwake.
“Bila shaka, kama hatutashinda, hilo ni wazi kabisa... lakini sijali kuhusu hilo,”alisema Amorim ambaye pia aliweka wazi kwamba hatua ya yeye kulipia tiketi wafanyakazi 30 kwa pesa zake baada ya klabu kusema haitowalipia ulikuwa ni juhudi ya kuinua morali.
Bosi wa Man United Sir Jim Ratcliffe anadaiwa kuzuia kuwalipia gharama za safari kwenda kutazama fainali Hipania wafanyakazi wa timu hiyo ikiwa ni mwendelezo wake wa kupunguza gharama za matumizi.
Baadhi ya wafanyakazi wanahofia pia wanaweza kukosa ajira zao ikiwa timu hiyo itashindwa kuchukua taji la Europa Lea-gue.