Hayuko sawa kisaikolojia

LONDON, ENGLAND.NYOTA kutoka Brazil, Richarlison amefichua siri kwamba anahitaji msaada wa kisaikolojia atakaporudi England baada ya kupitia changamoto nyingi katika maisha yake ya soka.
Fowadi huyo anayekipiga Tottenham alinaswa na kamera akitokwa na machozi baada ya kukosa bao na kutolewa nje katika ushindi wa mabao 5-0 dhidi ya Bolivia.

Pia, alianza katika mchezo mwingine dhidi ya Peru lakini alishindwa kufunga katika ushindi wa baao 1-0 .
Sasa Richarlison amecheza mechi nne za mwisho za Brazil bila ya kucheka na nyavu jambo ambalo limempatia wakati mgumu, hivyo anataka msaada wa kisaikojilia kwani hali hiyo inamtesa sana.

Aidha fowadi huyo amepitia changmoto kama hizo ndani ya miezi 12 akiwa Tottenham kwani amefunga mabao manne katika mechi 40 alizocheza.

Licha ya Kocha wa Spurs, Ange Postecoglou kumpanga katika mechi tatu za Ligi Kuu England msimu huu fowadi huyo ameshindwa kucheka na nyavu.

Sasa fowadi huyo amefunguka kuhusu changamoto zinazomkabili na kuvumilia: "Nahitaji msaada haraka wa kisaikolojia inaniumiza sana, akili yangu inatakiwa kufanya kazi, nikiwa uwanjani najaribu kufurahi na wachezaji wenzangu, napambana kwa ajili ya timu, wakati mwingine mambo hayaendi kama ninavyotarajia, nadhani haya mambo yanachangiwa na ishu binafsi nje ya uwanja. Hata kama nataka mambo yangu yaende sawa, mwisho wa siku yanaenda tofauti."

Richarlison aliondolewa katika kikosi kilichocheza ligi dhidi ya Burnley, katika mchezo huo, Son Heung-min alifunga hat-trick katika ushindi wa mabao 5-2.