Geremi Njitap ampa maua yake Cole Palmer akimfanisha na Lampard
Muktasari:
- Kwa mujibu wa mchezaji huyo wa zamani wa kikosi cha Cameroon, amesema wawili hao ni wafungaji bora, ingawa Palmer ni mchezaji wa kushambulia zaidi.
Kiungo wa zamani wa Chelsea, Geremi Njitap, amemlinganisha gwiji wa klabu hiyo, Frank Lampard na kinda anayetamba kwa sasa, Cole Palmer.
Kwa mujibu wa mchezaji huyo wa zamani wa kikosi cha Cameroon, amesema wawili hao ni wafungaji bora, ingawa Palmer ni mchezaji wa kushambulia zaidi.
Amesema Palmer amekuwa mchezaji wa kiwango cha kushangaza tangu alipojiunga na The Blues akitokea Manchester City mwaka 2023, hivyo anatarajia mambo mengi kutoka kwake kutokana na umri mdogo alionao.
Mchezaji huyo wa kimataifa wa England, tayari ameshatwaa baadhi ya mataji akiwa na Chelsea, ikiwemo Kombe la Dunia la Klabu (FIFA Club World Cup).
Akizungumza na FourFourTwo, Njitap amesema: “Frank Lampard na Cole Palmer wote ni wafungaji wa mabao. Wanaweza kufunga wakati wowote ndani ya mchezo. Ukiangalia jinsi Frank alivyokuwa akicheza, alikuwa namba nane, mwenye sifa ya kucheza ‘box to box’.
“Palmer ni mchezaji wa kushambulia zaidi, lakini ana ubora mkubwa wa kiufundi. Palmer alikuwa na kiwango cha kushangaza wakati wa mechi ya fainali ya Kombe la Dunia la Klabu. Nilishangaa sana. PSG ilikuwa timu ya kuogopwa, ilikuwa inashinda kila kitu. Lakini, Chelsea ilishinda kwa kishindo.”