Gabriel azua wasiwasi mkubwa Arsenal
Muktasari:
- Beki huyo hajashiriki vipindi vya mazoezi yote tangu alipotolewa uwanjani akiwa na maumivu ya paja kwenye mechi ya ushindi wa mabao 4-0 dhidi ya Atletico Madrid kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya, Jumanne iliyopita.
LONDON, ENGLAND: BEKI wa kati wa Arsenal, Mbrazili, Gabriel amezua wasiwasi mkubwa kwenye timu hiyo kutokana na hali yake ya kiafya inayomfanya kocha Mikel Arteta asiwe na uhakika wa kumtumia.
Beki huyo hajashiriki vipindi vya mazoezi yote tangu alipotolewa uwanjani akiwa na maumivu ya paja kwenye mechi ya ushindi wa mabao 4-0 dhidi ya Atletico Madrid kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya, Jumanne iliyopita.
Jambo hilo limemfanya kocha Arteta kuwa na wasiwasi kabla ya chama lake halijakabiliana na Crystal Palace kwenye mchezo wa Ligi Kuu England uwanjani Emirates, Jumapili.
Gabriel amekuwa na mchango mkubwa sana katika kikosi cha Arsenal akifunga mabao na kukaba, ambapo timu hiyo hadi sasa imeruhusu mabao matatu tu katika mechi nane ilizocheza kwenye Ligi Kuu England.
Kocha Arteta hajakata tamaa moja kwa moja, akiamini Gabriel anaweza kuwa fiti na kucheza mechi hiyo ya Palace, aliposema: “Gabi aliondoka uwanjani akiwa na tatizo na ameshindwa kufanya mazoezi tangu siku ile, hivyo tutamchunguza kwa ukaribu zaidi kuona kama anaweza kucheza kwenye mechi za wikiendi hii au la.”
Arteta alipuuzia habari za kwamba unapokuwa na safu nzuri ya ulinzi inakuweka kwenye uwezekano mkubwa wa kubeba ubingwa baada ya kulinganisha Arsenal ya msimu uliopita kwamba ilikosa ubingwa mbele ya Liverpool licha ya kufungwa mabao machache kuliko hata timu hiyo ya Anfield iliyofanikiwa kunyakua taji hilo.
Arteta amesema: “Sawa, tunataka rekodi za aina hiyo kama zitaweza kuleta mataji, lakini nadhani tunahitaji kupambana zaidi katika nafasi zote ili kufikia mafanikio tunayotaka."