Gabriel azua presha Arsenal
Muktasari:
- Beki huyo wa kati, ambaye ni moyo wa safu ya ushindi ya Arsenal chini ya kocha Mikel Arteta, alioenakana akiwa hana raha ndani ya uwanja wakati wa mchezo kabla ya kuonyesha ishara kwa benchi la ufundi na hivyo kutolewa uwanjani.
LONDON, ENGLAND: ARSENAL inakabiliwa na pigo kubwa hasa katika kuelekea kipute chao cha North London derby baada ya beki wa kati Gabriel Magalhaes kulazimika kutoka uwanjani kwenye mechi ya kimataifa baina ya Brazil na Senegal.
Beki huyo wa kati, ambaye ni moyo wa safu ya ushindi ya Arsenal chini ya kocha Mikel Arteta, alioenakana akiwa hana raha ndani ya uwanja wakati wa mchezo kabla ya kuonyesha ishara kwa benchi la ufundi na hivyo kutolewa uwanjani.
Gabriel, 27, alitolewa uwanjani kipindi cha pili na nafasi yake kuingizwa Wesley, kuliacha benchi la ufundi la Brazil kuguswa na sakata hilo, huku mashabiki wa Arsenal wakiwa kwenye hofu.
Gabriel alionekana akitembea kwa kuchechemea wakati anakwenda benchini, huku Kocha wa Brazil, Carlo Ancelotti akisema mchezaji huyo alisumbuliwa na maumivu ya misuli ya paja kwa upande wa ndani.
Ancelotti amesema: “Majeraha mabaya? Bado sifahamu, amekuwa na tatizo la maumivu upande wa ndani wa paja lake na madaktari watamfanyia uchunguzi zaidi. Tunampa pole sana kwa hili na hakika tumehuzunika, mchezaji anapopata majeraha, nadhani atapona haraka.”
Kukosekana kwa Gabriel kunakuja kwenye kipindi kigumu kwa Arsenal, wakati huu ikikabiliwa na mechi dhidi ya mahasimu wao Spurs katika mchezo ujao wa Ligi Kuu England utakaochezwa baada ya kumalizika kwa mapumziko ya mechi za kimataifa.
Kocha Arteta amekuwa akitegemea sana pacha ya mabeki Gabriel na William Saliba, ambao wamekuwa na kiwango bora katika kuisaidia timu hiyo kufikia malengo yake.
Katika mechi hiyo ya kimataifa ya kirafiki, Brazil iliichapa Senegal 2-0, huku mabao hayo uakifungwa na winga mpya wa Chelsea, Estevao na kiungo wa Manchester United, Casemiro.