FA yatuliza hofu England
Muktasari:
- Baada ya ushindi huo, Tuchel hakusita kukosoa kiwango cha timu yake akisema walikuwa na bahati kubwa ya kushinda kutokana na makosa ya wapinzani pamoja na msaada wa VAR.
LOS ANGELES, MAREKANI: ENGLAND ilikata tiketi ya kucheza nusu fainali ya Kombe la Dunia baada ya kuichapa Norway kwa ushindi wa mabao yaliyopatikana baada ya dakika za nyongeza katika mchezo uliochezwa kwenye joto kali la Miami, lakini kilichozua gumzo zaidi ni tofauti ya kauli kati ya kocha Thomas Tuchel na nyota Jude Bellingham.
Baada ya ushindi huo, Tuchel hakusita kukosoa kiwango cha timu yake akisema walikuwa na bahati kubwa ya kushinda kutokana na makosa ya wapinzani pamoja na msaada wa VAR.
“Tulikuwa na bahati. Tulifanya makosa mengi ya kiufundi na kimkakati, hatukuwa na kasi ya kutosha na tulijitengenezea mazingira magumu,” alisema kocha huyo Mjerumani.
Hata hivyo, Bellingham ambaye aliifungia England mabao mawili na kufikisha jumla ya sita kwenye michuano hiyo, alionekana kutofautiana na bosi wake.
“Labda ana hoja zake, lakini huenda hajui ilivyo vigumu kucheza kwenye hali ya hewa kama hii dhidi ya wachezaji wa kiwango cha Erling Haaland, Martin Odegaard, Antonio Nusa na Alexander Sorloth. Si mchezo rahisi,” alisema kiungo huyo wa Real Madrid.
Bellingham alisisitiza kuwa wakati mwingine timu kubwa hailazimiki kucheza soka la kuvutia ili ishinde.
“Huwezi kushinda kila mechi kwa kupiga pasi 1,000. Wakati mwingine unapaswa kushinda kwa mapambano, na ndiyo tulichofanya.”
Licha ya kauli hizo kuonekana kama mgongano wa wazi, viongozi wa Chama cha Soka England (FA) wameeleza kuwa hakuna mgogoro wowote kati ya Tuchel na Bellingham.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka ndani ya kambi ya England, kauli hizo zilitokana na hisia za mara baada ya mchezo mgumu, huku Bellingham akidaiwa kutokuwa amesikia maelezo yote aliyoyatoa kocha wake. Baadaye Tuchel alimiminia sifa kiungo huyo.
“Alitoa kiwango cha dunia kutoka kwa mchezaji wa kiwango cha dunia. Alifanya maamuzi makubwa katika nyakati muhimu kabisa. Amecheza vizuri sana,” alisema. England itavaana na Argentina kwenye mchezo wa nusu fainali, wakati mchezo mwingine utakuwa kati ya Hispania na Ufar ansa.