Mbappe, Yamal wabeba matumaini nusu fainali
Muktasari:
- Kwa mujibu wa takwimu za Opta, hii ni mara ya pili pekee kwa mataifa hayo kukutana kwenye Kombe la Dunia. Mara ya kwanza ilikuwa mwaka 2006 katika hatua ya 16 Bora, ambapo Ufaransa ilitoka nyuma na kushinda mabao 3-1.
BOSTON, MAREKANI: USIKU wa leo macho ya dunia yataelekezwa kwenye nusu fainali ya Kombe la Dunia 2026, ambapo mabingwa wa zamani Ufaransa na Hispania watavaana katika mechi inayotarajiwa kuwa ya kiwango cha juu kutokana na historia, ubora wa vikosi na rekodi walizoweka kuelekea hatua hii.
Kwa mujibu wa takwimu za Opta, hii ni mara ya pili pekee kwa mataifa hayo kukutana kwenye Kombe la Dunia. Mara ya kwanza ilikuwa mwaka 2006 katika hatua ya 16 Bora, ambapo Ufaransa ilitoka nyuma na kushinda mabao 3-1.
Hata hivyo, katika miaka ya hivi karibuni Hispania imekuwa ikipewa nafasi kubwa zaidi kwenye rekodi za ana kwa ana. Kati ya mechi 10 za mwisho katika mashindano yote, La Roja imeshinda saba, sare moja na kupoteza mara mbili pekee dhidi ya Les Bleus.
Katika mikutano miwili ya mwisho, Hispania imeibuka mshindi baada ya kushinda 2-1 kwenye nusu fainali ya Euro 2024 kabla ya kuifunga Ufaransa mabao 5-4 katika UEFA Nations League mwezi Juni 2025.
Ufaransa bingwa wa nusu fainali
Ufaransa imefika hatua ya nusu fainali ya Kombe la Dunia kwa mara ya nane katika historia yake, ikiwa nyuma ya Ujerumani pekee iliyofika mara 12.
Baada ya kupoteza nusu fainali zake tatu za kwanza mwaka 1958, 1982 na 1986, Les Bleus imefuzu fainali katika kila nusu fainali nne zilizopita mwaka 1998, 2006, 2018 na 2022.
Cha kuvutia zaidi ni kwamba ilishinda nusu fainali tatu zilizopita bila kuruhusu bao hata moja.
Kwa upande wa Hispania, hii ni mara ya pili pekee kucheza nusu fainali ya Kombe la Dunia. Mara ya kwanza ilikuwa mwaka 2010, ambapo iliendelea kutwaa ubingwa wa dunia.
Katika mashindano makubwa (Kombe la Dunia na Euro), Hispania imevuka hatua ya nusu fainali mara sita kati ya saba zilizopita, huku kipigo chake pekee kikitokea dhidi ya Italia kwa mikwaju ya penalti kwenye Euro 2020.
Rekodi kubwa ziko hatarini
Iwapo Ufaransa itashinda leo, itakuwa taifa la tatu tu katika historia kufuzu fainali tatu za Kombe la Dunia mfululizo, baada ya Ujerumani (1982, 1986 na 1990) pamoja na Brazil (1994, 1998 na 2002).
Les Bleus pia imeshinda mechi zote sita ilizocheza kwenye Kombe la Dunia 2026. Ushindi mwingine utaifanya kuwa timu ya pili ya Ulaya kushinda mechi saba mfululizo kwenye Kombe la Dunia, baada ya Italia iliyofanya hivyo kati ya 1934 na 1938.
Kwa upande wa Hispania, tangu mwaka 2018 imepoteza mechi moja tu kati ya 27 katika mashindano makubwa, ikishinda 16 na kutoka sare mara 10.
Tangu ilipopoteza 2-1 dhidi ya Japan kwenye Kombe la Dunia 2022, Hispania haijafungwa katika mechi 14 mfululizo, ikiruhusu mabao matano pekee huku ikimaliza mechi tisa bila kuruhusu bao.
Aidha, La Roja imeshinda mechi zake saba zilizopita za hatua ya mtoano kwenye mashindano makubwa na inaweza kuweka rekodi mpya ya Ulaya kwa kufikisha ushindi nane mfululizo.
Mbappé moto
Safu ya ushambuliaji ya Ufaransa imekuwa kali zaidi kwenye Kombe la Dunia 2026.
Les Bleus imepiga mashuti 47 yaliyolenga lango, idadi kubwa zaidi tangu ilipopiga 53 kwenye Kombe la Dunia 1998.
Nahodha Kylian Mbappé ndiye kinara akiwa na wastani wa mashuti 3.3 yaliyolenga lango kwa kila dakika 90.
Mbappé na Ousmane Dembélé wameonyesha ushirikiano mkubwa, wakitengenezeana nafasi 19 za mabao kwenye Kombe la Dunia.
Endapo wataongeza nafasi moja tu, wataingia kwenye orodha ya jozi nne bora zaidi kuwahi kushirikiana kwa kiwango hicho katika historia ya mashindano tangu mwaka 1966.
Mbappé pia anasaka bao lake la kwanza kabisa katika hatua ya nusu fainali ya Kombe la Dunia, licha ya kuwa tayari ana mabao 12 kwenye hatua nyingine za mtoano.
Deschamps avunja rekodi
Kocha wa Ufaransa, Didier Deschamps, ataiongoza timu yake katika mechi ya 26 ya Kombe la Dunia, rekodi mpya kwa makocha wote katika historia ya mashindano hayo.
Chini yake, Mbappé amecheza mechi 20 za Kombe la Dunia na kufunga mabao 20, rekodi ya juu zaidi kwa mchezaji akiwa chini ya kocha mmoja.
Kwa upande wa Hispania, kocha Luis de la Fuente anaendelea kuwa na rekodi ya kuvutia, akiwa hajapoteza hata mechi moja katika Kombe la Dunia na Euro ndani ya michezo 13 aliyosimamia, akishinda 12 na kutoka sare moja.
Merino silaha ya benchi
Kiungo Mikel Merino ameandika historia kwa kuwa mchezaji wa kwanza kufunga mabao ya ushindi katika mechi mbili tofauti za hatua ya mtoano ya Kombe la Dunia akiwa ametokea benchi.
Aliifanyia hivyo dhidi ya Ureno na baadaye dhidi ya Ubelgiji, jambo linaloonyesha jinsi benchi la Hispania linavyoweza kubadili matokeo ya mchezo wakati wowote.
Kwa rekodi, kila upande una sababu za kujiamini. Ufaransa inabeba uzoefu mkubwa wa hatua hii, huku Hispania ikiingia na mwendelezo wa matokeo mazuri na rekodi bora katika miaka ya karibuni. Ni pambano la vigogo ambalo lina kila sifa ya kuwa fainali kabla ya fainali.