Enzo Fernandez aomba kuondoka Chelsea
Muktasari:
- Fernández ni mmoja kati ya viungo muhimu wa Chelsea akionyesha kiwango bora tangu alipojiunga nao, lakini hivi karibuni amekuwa na sintofahamu na klabu hiyo baada ya kauli zake za utata zinazoashiria kwamba anataka kutua Real Madrid.
KIUNGO wa kimataifa wa Argentina, Enzo Fernandez, 25, anayekipiga Chelsea anaripotiwa kujiandaa kuwasilisha ombi la kuondoka katika dirisha lijalo la majira ya kiangazi.
Fernández ni mmoja kati ya viungo muhimu wa Chelsea akionyesha kiwango bora tangu alipojiunga nao, lakini hivi karibuni amekuwa na sintofahamu na klabu hiyo baada ya kauli zake za utata zinazoashiria kwamba anataka kutua Real Madrid.
Kauli zake zilisababisha afungiwe mechi mbili kama sehemu ya adhabu jambo lililosababisha wakala wake kutoka hadharani na kusema klabu hiyo imemuonea mchezaji wake.
Inaelezwa Real Madrid imeshaanza kuzungumza na wakala wa Enzo na ipo tayari kutoa kiasi cha pesa kinachohitajika ili kufanikisha dili hilo. Hata hivyo, matajiri hao hawahitaji kujitokeza hadharani kwa sasa kwani wanaona itakuwa ngumu kwa Chelsea kukubali kumuuza.
James Trafford
TOTTENHAM Hotspur inafikiria kumsajili kipa wa Manchester City na timu ya taifa ya England, James Trafford, 23, kutoka Manchester City katika dirisha lijalo la majira ya kiangazi ili awe mbadala wa Guglielmo Vicario anayetarajiwa kuondoka. Vicario, 29, anaripotiwa kuwa ameshafanya makubaliano ya kutua Inter Milan, hali inayoilazimisha Spurs kuanza kutafuta mbadala wake. Trafford yupo fiti sana kwa sasa.
Harry Maguire
BEKI wa Manchester United na timu ya taifa ya England, Harry Maguire, 33, alikataa ofa ya kujiunga na Inter Miami kabla ya kusaini mkataba mpya wa kuendelea kualia Old Trafford. Inaelezwa kuwa Maguire ana nia ya kumalizia maisha yake ya soka akiwa Manchester United, akiamini bado ana mchango mkubwa ndani ya kikosi hicho. Awali ilionekana kuwa huenda staa huyu angemaliza ndoa yake ya muda mrefu na Man U.
Marco Palestra
LIVERPOOL imejiunga na Newcastle United katika harakati za kumfuatilia beki wa kimataifa wa Italia, Marco Palestra, 21, ambaye kwa sasa yuko kwa mkopo katika Cagliari akitokea Atalanta. Palestra ambaye anacheza kama beki wa kulia ameendelea kuonyesha kiwango bora kutokana kwa msimu huu hali iliyovutia maskauti wengi wa timu kubwa za Ulaya ambao wamekuwa Italia kumtazama.
Manuel Ugarte
MANCHESTER United inatarajiwa kumuachia kiungo wa kimataifa wa Uruguay, Manuel Ugarte, 24, katika dirisha lijalo la majira ya kiangazi. Klabu kadhaa tayari zinaonyesha nia ya kumsajili ikiwa ni pamoja na Galatasaray, Newcastle United na Tottenham Hotspur. Ugarte ambaye hapati nafasi ya kutosha kwa sasa katika kikosi cha kwanza cha Man United anaweza kuuzwa kwa takribani Pauni 40 milioni.
Yves Bissouma
FENERBAHCE ina nia ya kumsajili kiungo wa Tottenham Hotspur, Yves Bissouma mwenye umri wa miaka 29 katika dirisha lijalo la majira ya kiangazi. Bissouma, ambaye ni mchezaji wa kimataifa wa Mali amekuwa hapati nafasi ya kutosha msimu huu ambapo amecheza mechi nane pekee jambo linalochochea kutaka atafute changamoto mpya mahali kwingineko. Fenerbahce ipo tayari kumchukua hata kwa mkopo.
Elliot Anderson
MANCHESTER United inaonekana kuwa katika hatari ya kumkosa kiungo wa Nottingham Forest na timu ya taifa ya England, Elliot Anderson, 23, ambaye anadaiwa kupendelea zaidi kujiunga na majirani zao Manchester City. Anderson ameibuka kuwa mmoja wa viungo wanaowindwa zaidi kwa sasa nchini England kutokana na kiwango bora anachoonyesha akiwa na Forest.
Marc Casado
KIUNGO wa Barcelona, Marc Casado, 22, yupo tayari kuondoka katika klabu hiyo kwenye dirisha lijalo la majira ya kiangazi baada ya kupoteza nafasi katika kikosi cha kwanza. Casado ambaye ni mchezaji wa kimataifa wa Hispania, amekuwa akikosa nafasi ya kucheza mara kwa mara, hali inayomfanya kufikiria kutafuta changamoto mpya ili kupata nafasi zaidi uwanjani. Uamuzi wake unaonekana unaweza kuvutia klabu nyingine kubwa.