England, Argentina ni vita ya kisasi
Muktasari:
- Simba watatu (Three Lions) walifuzu hatua ya nusu fainali baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Norway katika mchezo uliokwenda hadi dakika za nyongeza Jumamosi usiku.
NEW YORK, MAREKANI: ENGLAND italazimika kuiondoa Argentina ya Lionel Messi ikiwa inataka kuendelea kuota ndoto ya kutwaa Kombe la Dunia 2026.
Simba watatu (Three Lions) walifuzu hatua ya nusu fainali baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Norway katika mchezo uliokwenda hadi dakika za nyongeza Jumamosi usiku.
Kwa mara nyingine tena, Jude Bellingham alikuwa shujaa wa England baada ya kufunga mabao mawili muhimu yaliyowafanya mashabiki kuendelea kuamini kuwa huenda hatimaye kombe likarejea nyumbani.
Hata hivyo, sasa kikosi cha kocha Thomas Tuchel kinakabiliwa na mtihani mkubwa zaidi wa kumenyana kwa mara ya kwanza kabisa na Lionel Messi katika mechi ya kimataifa.
Messi na Argentina walinusurika
Mabingwa watetezi, Argentina, nao walihitaji dakika 120 ili kuiondoa Uswisi kwa ushindi wa mabao 3-1, katika mchezo uliogubikwa na utata baada ya mshambuliaji wa Uswisi, Breel Embolo, kuonyeshwa kadi nyekundu.
Sasa macho ya dunia yataelekezwa kwenye pambano hilo la kihistoria kati ya mataifa mawili yenye uhasama mkubwa katika soka la dunia.
England na Argentina hazijakutana tangu mwaka 2005, kipindi ambacho Messi alikuwa bado hajaanza kujijengea jina kubwa na hakuwamo kwenye kikosi cha Argentina.
Historia ya vita vya England na Argentina
Mechi kati ya mataifa haya mawili zimewahi kuandika sura muhimu katika historia ya Kombe la Dunia.
Mwaka 1986, Diego Maradona aliiondoa England kwa bao lake maarufu la "Hand of God", kabla ya kuongeza bao jingine linalotajwa kuwa miongoni mwa bora zaidi kuwahi kufungwa katika historia ya mchezo.
Miaka 12 baadaye, kwenye Kombe la Dunia la 1998, England ilitolewa kwa mikwaju ya penalti baada ya David Beckham kuonyeshwa kadi nyekundu kufuatia kumchezea rafu Diego Simeone.
Hata hivyo, England pia ina kumbukumbu tamu dhidi ya Argentina. Iliifunga katika safari yake ya kutwaa Kombe la Dunia mwaka 1966, na baadaye Beckham akalipiza kisasi kwa kufunga penalti ya ushindi katika hatua ya makundi ya Kombe la Dunia 2002.
Tiketi ya fainali ipo mezani
Pambano la Jumatano litakuwa na uzito mkubwa, kwani mshindi atatinga fainali ya Kombe la Dunia itakayopigwa jijini New York Jumapili ijayo.
Atakayeshinda kati ya England na Argentina atakutana na mshindi wa nusu fainali nyingine kati ya Ufaransa na Hispania, huku dunia ikisubiri kuona kama Bellingham ataendelea kung'ara au Messi ataandika historia nyingine katika safari yake ya mwisho ya Kombe la Dunia.