Davido aipa Taifa Stars bao dhidi ya Nigeria
Muktasari:
- Hata hivyo, Davido ameshindwa kutoa maelezo ya kina kwenye uchaguzi wake huo, huku jambo hilo likiibua mjadala mzito kwenye mitandao ya kijamii.
RABAT, MOROCCO: STAA wa muziki wa Nigeria, Davido ametoa utabiri wake wa nchi ambayo anaamini itanyakua ubingwa wa Afcon 2025.
Hata hivyo, Davido ameshindwa kutoa maelezo ya kina kwenye uchaguzi wake huo, huku jambo hilo likiibua mjadala mzito kwenye mitandao ya kijamii.
Mkali huyo wa Afrobeats alifika mbali kwa kutabiri Nigeria ndiyo itakayonyakua ubingwa na itaichapa Morocco kwenye mechi ya fainali kwa mabao 3-0.
Mwimbaji huyo ambaye alifanya shoo kwenye ufunguzi wa Afcon 2025, alibainisha matumaini yake kwa Nigeria, ambayo anaamini itashinda mechi yake ya kwanza kwenye Kundi C itakapomenyana na Tanzania.
Kwenye hilo, Davido alibeti kabisa kuweka mkwanja mrefu akiamini Nigeria itaichapa Tanzania, aliposema "Uthubutu mkubwa, mavuno makubwa."
Davido alitumia ukurasa wake wa X akionyesha picha ya mkeka wake. Kwenye mkeka huo, Davido alichagua "Both Teams to Score" (BTTS), kwa maana ya timu kufungana na hilo likitokea, basi atakuwa na uhakika wa kushinda Dola 96,564.
Super Eagles itakipiga na Tanzania katika uwanja wa Complex Sportif de Fes, Morocco, mechi itakayokuwa ya kwanza kwa timu hiyo kwenye Kundi C katika msako wao huo wa kuwania ubingwa wa Afrika.