Big Six yatishiwa kupokwa pointi 30

LONDON, ENGLAND. KLABU za Big Six Ligi Kuu England zimekubali kulipa faini ya Pauni 3.5 milioni kila moja baada ya kujaribu kuanzisha michuano ya European Super League.

Lakini, miamba hiyo Arsenal, Chelsea, Liverpool, Tottenham, Manchester United na Manchester City zitakabiliana na faini ya Pauni 20 milioni na kupunguziwa pointi 30 kama zitarudi tena kujiunga kwenye michuano hiyo iliyoanzishwa na klabu 12 vigogo vya Ulaya, huku Barcelona, Real Madrid na Juventus zikibaki wenyewe na bado hazijatangaza kujitoa.

Timu nyingine zilizojitoa pamoja na za Big Six ni AC Milan, Inter Milan na Atletico Madrid. Klabu hizo za EPL zitatanguliwa kulipa Pauni 1.44 milioni, pamoja na asilimia tano ya mapato yao Ligi ya Mabingwa Ulaya, Europa League au Europa Conference League watakayolipwa kwa ajili ya msimu ujao. Adhabu inaweza kuwa kali zaidi na pengine kulipa hadi Pauni 43.5 milioni kama wataamua kujiunga na ligi nyingine yoyote ya mtindo kama huo kwa siku za baadaye.