Bayern Munich yafukuzia rekodi Bundesliga
Muktasari:
- Bayern inaongoza ligi kwa tofauti ya pointi tisa huku kukiwa kumebaki michezo saba na tayari imefunga mabao 97, manne tu kufikia rekodi ya mabao 101 iliyowekwa msimu wa 1971/72.
BERLIN, UJERUMANI: MABINGWA watarajiwa Bayern Munich inaendelea kuwasha moto kwenye Bundesliga ikisaka kuweka rekodi mpya ya mabao msimu huu.
Bayern inaongoza ligi kwa tofauti ya pointi tisa huku kukiwa kumebaki michezo saba na tayari imefunga mabao 97, manne tu kufikia rekodi ya mabao 101 iliyowekwa msimu wa 1971/72.
Chini ya Kocha Vincent Kompany, timu hiyo inaonekana kuwa kwenye kasi ya kuvunja rekodi hiyo, huku mshambuliaji Harry Kane naye akiwinda rekodi ya Robert Lewandowski ya kufunga mabao 41 katika msimu mmoja.
Kane tayari ana mabao 31 msimu huu licha ya kusumbuliwa na majeraha, akisaidiwa na Luis Diaz mwenye mabao 15, huku Michael Olise aking’ara kwa pasi za mwisho 17 zilizosababisha mabao 11.
Hata hivyo, Bayern inakabiliwa na ratiba ngumu, ikianza na mechi dhidi ya SC Freiburg, ambayo inapigania nafasi za kushiriki michuano ya Ulaya.
Freiburg ipo nafasi ya nane na pointi 37, ikisaka kumaliza ndani ya sita bora ili kufuzu UEFA Europa Conference League.
Bayern pia inajiandaa na kibarua kizito cha kukutana na Real Madrid katika Ligi ya Mabingwa Ulaya wiki ijayo, jambo linalofanya kila mechi kuwa ya muhimu kwao katika harakati za kumaliza msimu kwa mafanikio makubwa.