Arsenal, Napoli zaangukia pua Europa

LONDON, ENGLAND.
VIGOGO wameanza vibaya kule Europa League baada ya jana Alhamisi Arsenal kutoka sare mbele ya Benfica kule Ureno na Napoli kuchapwa mabao mawili pale Hispania.

Michezo hiyo ilikua ni ya hatua ya mtoano ya 32 bora ambapo huchezwa nyumbani na ugenini na timu itakayopita itaingia hatua ya 16 bora.

Benfica ndio ilikua ya kwanza kupata bao dakika ya 55 kwa mkwaju wa penati uliopiga na Pizzi, lakini dakika mbili baadae yani 57, Bukayo Saka aliisawazishia Arsenal kwa pasi ya Cedric Soares.

Kwa upande wa Napoli yenyewe ilikubali kuruhusu mabao mawili ndani ya dakika tatu, ikiwa ni dakika ya 19 lililofungwa na Yangel Herrera kabla ya Kenedy kutia kamba ya pili kwa pasi ya Darwin Machis dakika ya 21.

Mechi nyingine zilizopigwa jana, ilikuwa ni Ajax iliyoshinda 2-1 mbele ya Lille Maccabi Tel Aviv ikiwa nyumbani ikakubali kichapo cha mabao 2-1 mbele ya FC Shakhtar Donetsk, huku Molde na Hoffenheim zikitoka sare ya 3-3.
Royal Antwerp FC ya Ubelgiji iliambulia kipigo cha aibu kutoka kwa vijana wa Steven Gerrard, Rangers kwa kufungwa mabao 4-3.

Salzburg alipowahi kupita straika wa sasa wa Borussia Dortmund, Erling Braut Haaland ilikubali kulala kwa mabao 2-0 dhidi ya Villarreal.

Mechi za marudiano  zinatarajiwa kupigwa Februari 25 isipokuwa Wolfsberg na Tottenham ambazo mechi yao itapigwa February 24, ili kufuata kanuni za michuano zinaeleza kwamba mechi mbili haziwezi kuchezwa ndani ya siku moja kwenye mji mmoja.

Spurs makao yake ni pale London na Arsenal pia makazi yake ni pale London.