Arsenal kuondoka uwanja wa Emirates
Muktasari:
- Kwa mujibu wa tovuti ya City AM, mabosi wa Arsenal wameamua kuwasiliana na kampuni hiyo ambayo ndio ilibuni mchoro wa Emirates miaka ya nyuma.
LONDON, ENGLAND: VINARA wa Ligi Kuu England, Arsenal FC wanafikiria mpango wa kutotumia Uwanja wa Emirates kwa muda ili kuufanyia marekebisho yatakayoufanya kuwa wa pili kwa ukubwa kumilikiwa na timu za Ligi Kuu England.
Arsenal inadaiwa kuwa katika mazungumzo na kampuni maarufu ya usanifu majengo ya Populous ili kuipa kazi ya kuupanua au kuufanyia maboresho makubwa Uwanja wa Emirates.
Kwa mujibu wa tovuti ya City AM, mabosi wa Arsenal wameamua kuwasiliana na kampuni hiyo ambayo ndio ilibuni mchoro wa Emirates miaka ya nyuma.
Kampuni hiyo pia inajulikana kwa kubuni viwanja maarufu kama Wembley pamoja na wa Tottenham Hotspur FC, inadaiwa sasa itakuwa na kazi ya kuhakikisha inachora mchoro wenye ubora ili kufikiwa viwango ambavyo Arsenal inavihitaji.
Ripoti zinaeleza upanuzi huo unaweza kuongeza uwezo wa uwanja huo hadi kubeba zaidi ya mashabiki 70,000, jambo ambalo litakuwa ni suluhisho la mashabiki wengi kulalamika kwamba wamekosa tiketi katika mechi kadhaa.
Kwa mujibu wa ripoti, pendekezo hilo la kuukarabati uwanja huo linaweza kuhusisha kazi kubwa za ujenzi ambazo zinaweza kulazimisha kikosi cha Mikel Arteta kuhamia uwanja mwingine kwa muda wakati maboresho yakifanyika.
Kwa sasa Uwanja wa Emirates una uwezo wa kubeba mashabiki takribani 60,000, ambao wanaonekana kuwa hawatoshi kutokana na mahitaji ya sasa.
Arsenal itakuwa inaungana na Manchester United, ambao wapo katika mchakato wa kuboresha dimba la Old Trafford lenye uwezo wa kubeba mashabiki 75,000, kuwa na uwezo wa kuchukua mashabiki 100,000.
Hata hivyo, licha ya kujengwa kwa takribani miaka 22 iliyipita, Emirates bado unaonekana kama moja ya viwanja vya kisasa zaidi duniani.