Argentina yaichapa England dakika za jioni, yatinga fainali Kombe la Dunia 2026
Muktasari:
- England ilikuwa na dakika chache tu za kufuzu fainali yake ya kwanza ya Kombe la Dunia tangu mwaka 1966 lakini ilishindwa kulinda uongozi wake na kuadhibiwa na Argentina katika dakika za mwisho za mchezo.
ATLANTA, MAREKANI: TIMU ya taifa la Argentina imeonyesha kwa mara nyingine kwa nini ni mabingwa watetezi wa Kombe la Dunia baada ya kupindua matokeo na kuifunga England mabao 2-1 katika mchezo wa nusu fainali uliochezwa usiku wa Julai 15, 2026.
England ilikuwa na dakika chache tu za kufuzu fainali yake ya kwanza ya Kombe la Dunia tangu mwaka 1966 lakini ilishindwa kulinda uongozi wake na kuadhibiwa na Argentina katika dakika za mwisho za mchezo.
Baada ya kipindi cha kwanza kumalizika kwa matokeo ya 0-0, England ilianza kipindi cha pili kwa kasi na kufunga bao dakika ya 55 kupitia Anthony Gordon aliyemalizia pasi ya Morgan Rogers na kuwapa matumaini makubwa mashabiki wa Three Lions.
Hata hivyo, baada ya bao hilo, England ilianza kucheza kwa kujilinda zaidi, jambo lililoipa Argentina nafasi ya kutawala mchezo na kuendelea kushambulia lango la Jordan Pickford.
Presha hiyo ilizaa matunda dakika ya 85 wakati Enzo Fernández alipofunga bao la kusawazisha kwa pasi safi ya nahodha Lionel Messi, aliyeendelea kuonyesha ubora wake katika hatua muhimu za mashindano hayo.
Mechi ilionekana itamalizika kwa sare dakika 90, lakini dakika ya pili ya zile za nyongeza, Messi alitoa pasi nyingine ya mwisho iliyomkuta Lautaro Martínez ambaye hakufanya makosa na kufunga bao la ushindi lililowanyamazisha mashabiki wa England waliokuwa wamejaa katika Uwanja wa Atlanta.
Ushindi huo unaifanya Argentina kufuzu fainali ya pili mfululizo ya Kombe la Dunia, ikiwa na nafasi ya kutetea ubingwa wake dhidi ya Hispania katika mchezo wa fainali utakaochezwa Jumapili ya Julai 19, 2026 mjini New Jersey, Marekani.
Kwa upande wa England, ni maumivu mengine katika hatua ya nusu fainali baada ya kushindwa tena licha ya kuwa mbele kwa bao 1-0. Mara ya mwisho England ilipoteza nusu fainali ya Kombe la Dunia baada ya kuongoza ilikuwa mwaka 2018 ilipofungwa 2-1 na Croatia.
Takwimu zinaonyesha England ilipiga mashuti matano pekee katika mchezo huo, idadi ndogo zaidi kwao katika mechi yoyote ya Kombe la Dunia 2026, huku Argentina ikionekana kutawala sehemu kubwa ya mchezo baada ya mapumziko ya kunywa maji.
Baada ya mchezo, mshambuliaji wa zamani wa England, Wayne Rooney, amesema timu hiyo ilijirudisha nyuma mapema baada ya kupata bao na kuiruhusu Argentina kuamini inaweza kurejea.
"Tulikuwa katika nafasi nzuri sana, lakini baada ya kuongoza hatukujua cha kufanya. Tulikaa nyuma, tukawaruhusu watushambulie na mwisho tukavunjika," amesema Rooney.
Naye Alan Shearer amekiri kuwa Argentina ilistahili ushindi kutokana na namna ilivyocheza kwa utulivu na kuendelea kushikilia mpango wake wa mchezo hadi mwisho.
Kwa ushindi huo, Argentina itaikabili Hispania katika fainali ya Kombe la Dunia 2026, huku England ikishuka dimbani kucheza mechi ya kusaka nafasi ya tatu dhidi ya Ufaransa.