Coutinho amdatisha Gerrard

Coutinho amdatisha Gerrard

LONDON, ENGLAND. KOCHA wa Aston Villa, Steven Gerrard anaamini Philippe Coutinho ataleta maajabu kwenye timu baada ya kufunga bao kwenye mechi yake ya kwanza dhidi ya Manchester United.

Coutinho amereja Ligi Kuu England baada ya miaka minne iliyopita, amemtengeza nafasi bao la kusawazisha lililofungwa na Jacob Ramsey kabla ya yeye kupachika bao dhidi ya Man United dakika 14 akiingia akitokea benchi, mchezo huo ukimalizika kwa sare ya mabao 2-2.

Kiungo huyo wa Kimataifa wa Brazil alikuwa na wakati mgumu tangu alipojiunga na Barcelona kwa kitita cha Pauni 142 milioni akitokea Liverpool mwaka 2018.

Akizungumza baada ya sare ya mabao 2-2 waliyopata dhidi ya mashetani wekundu, Gerrard amesema Coutinho amerudi kwa kishindo na kufunga bao ni jambo zuri kwa timu yake.

“Ameisaidia timu amefunga bao na kutengeneza nafasi ya kufunga, nadhani kiwango chake kitaanza kurudi taratibu kama alivyokuwa akicheza Liverpool, katika ubora wake Coutinho ni kati ya wachezaji wakali EPL, Barcelona ilitumia pesa nyingi kumsajili, nadhani atang’ara sana ni suala muda,” alisema Gerrard.