Pamba Jiji yaanza na Baraza ikipishana na kinara wa mabao ikiahidi kurudi upya
Muktasari:
- Pamba Jiji inadaiwa kuondokewa na mastaa wake waliokuwa wakianza kikosi cha kwanza wakiwamo kipa Yona Amos na kinara wa mabao Mathew Tegis na sasa inaanza kujitafuta upya kwa ajili ya msimu ujao.
Wakati Pamba Jiji ikianza maandalizi ya msimu ujao, vigogo wa timu hiyo wamemuwahi Kocha Mkuu, Francis Baraza kumsainisha mkataba wa mwaka mmoja, huku wakipishana na mkali wa mabao msimu uliopita.
Baraza raia wa Kenya alikuwa na mafanikio makubwa kikosini humo katika msimu uliopita alipoiongoza timu kumaliza nafasi ya saba kwenye msimamo wa Ligi Kuu Bara kwa pointi 36 huku ikionesha ushindani na soka bora.
Wakati Baraza akisalia kwa chama hilo la jijini Mwanza, habari za ndani ilizopata Mwanaspoti ni kuwa timu hiyo imepata pigo kwa kuondokewa na mastaa takribani 11 wa kikosi cha kwanza akiwamo kinara wa mabao Methew Tegis raia wa Kenya aliyetimkia Kagera Sugar iliyorejea Ligi Kuu.
Tegis ambaye alitua Pamba dirisha dogo msimu wa 2024-2025 kutokea Shabana FC ya Ligi Kuu nchini Kenya, alikuwa na kiwango bora akiwa miongoni mwa wachezaji watano vinara wa mabao Ligi Kuu Bara 2025-2026 alipofunga 11 ikiwamo hat trick moja.
Kuondoka kwa staa huyo pamoja kipa Yona Amos anayetajwa kumalizana na Singida Black Stars, huwenda ikawapa wakati mgumu timu hiyo msimu ujao katika kutengeneza muunganiko na ushindani.
Tayari Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limeshatangaza Ligi Kuu msimu ujao itaanza Agosti 14, 2026 likizitaka timu kuanza mapema maandalizi ikiwamo usajili uliofunguliwa Julai 6 na kutarajiwa kufungwa Agosti 15 ili kuendeleza thamani ya ligi hiyo iliyopo nafasi ya sita kwa ubora Afrika.
Mmoja wa vigogo wa Pamba Jiji, ameliambia Mwanaspoti kuwa licha ya kuwa pigo kuondokewa na baadhi ya mastaa wake, lakini wanaamini usajili watakaoufanya, timu itabaki na kiwango kilekile.
"Tumeanza kuingiza wachezaji wapya kutokana na waliokuwapo kuondoka, tayari tumemalizana na Kocha Baraza tukisubiri kuanzia wiki ijayo kushusha sura mpya.
"Ni kweli itatuathiri kuondokewa na wachezaji wengi ila tutasuka upya timu na kwakuwa kocha tunaye atatusaidia kutengeneza kikosi bora chenye ushindani na mvuto uleule," amesema kigogo huyo.