Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Mashabiki 18,000 kushuhudia Mashemeji Dabi, polisi 300 kulinda usalama

MASHEMEJI Pict

Muktasari:

  • Hii ni sawa na asilimia 78.6 ya uwezo wa Uwanja wa Nyayo uliokarabatiwa hivi karibuni, ambao unaweza kuchukua watazamaji 22,900 wote wakiwa wameketi.

Mashabiki 18,000 pekee wataruhusiwa kuingia Uwanja wa Nyayo, Jumapili Desemba 7, 2025 kushuhudia mechi ya Ligi Kuu ya Kenya kati ya mahasimu wa jadi, Gor Mahia na AFC Leopards, timu mwenyeji imebainisha.

Hii ni sawa na asilimia 78.6 ya uwezo wa Uwanja wa Nyayo uliokarabatiwa hivi karibuni, ambao unaweza kuchukua watazamaji 22,900 wote wakiwa wameketi.

Katibu Mkuu wa Gor Mahia, Nicanor Arum, amesema hatua hiyo inalenga kutimiza masharti ya Sports Kenya kwamba uwanja huo usijazwe hadi uwezo kamili kutokana na hatari kubwa ya mechi hiyo.

Arum pia amefichua kuwa klabu imelazimika kutimiza masharti kadhaa yaliyoainishwa na Sports Kenya, waendeshaji wa viwanja vya umma nchini, ili kuruhusiwa kuandaa mechi hiyo.

Sports Kenya imewahi kuzipiga marufuku na kuzipiga faini AFC Leopards na Gor Mahia hapo awali kutokana na uharibifu wa miundombinu yao unaohusishwa na mashabiki wakati wa mechi za Mashemeji Dabi.

“Baada ya kulipia matumizi ya uwanja, Sports Kenya walisisitiza tufanye mikutano mitatu ya maandalizi kabla ya Jumapili ili kukamilisha mipango ya uandikaji mechi. Tulifanya kikao cha kwanza Jumanne, na vingine vitafanyika Ijumaa na Jumamosi,” amesema Arum.

Mikutano hiyo ilihusisha Sports Kenya, AFC Leopards, Shirikisho la Soka Kenya (FKF), polisi, na wadau wengine.

Dabi ya Mashemeji Jumapili hii ambayo ni mechi ya 98 ya ligi kati ya watani hao wawili, awali ilipangwa kuchezwa wiki iliyopita lakini iliahirishwa kutokana na ukosefu wa uwanja unaofaa.

Tiketi zimeanza kuuzwa mtandaoni Jumatatu kwa bei ya Sh200 kawaida, Sh1,000 VIP na Sh5,000 VVIP.

“Tumeachana na uuzaji wa tiketi za karatasi,” amesema Arum.

“Tiketi zitauzwa mtandaoni pekee, na tutajitahidi kuhakikisha hakuna uuzaji wa tiketi siku ya mechi.”

Mashabiki wanaopanga kuendesha magari kwenda uwanjani watalipa Sh100 ya ziada kwa huduma ya maegesho. Arum amesisitiza kuwa klabu imeweka mipango madhubuti ya usalama wa magari.

Arum amesema wasimamizi 130 watatumika kutoa huduma za usalama na utulivu wakati wa mechi.

“Kutakuwa na wasimamizi 100 kutoka Gor Mahia na 30 kutoka AFC Leopards,” amebainisha.

Dabi ya Mashemeji iliyochezwa Nyayo Machi 30, 2025, ilijaa kupita uwezo, hali iliyozua hofu ya usalama, hivyo idadi ya mashabiki kwa mechi ya Jumapili itafuatiliwa kwa makini.

Arum amesema wameweka hatua za kutosha kuhakikisha udhibiti mzuri wa umati na usimamizi wa mashabiki.

“Kutakuwa na zaidi ya polisi 300 katika mechi ya Jumapili. Maafisa hao watatoka vitengo mbalimbali ikiwemo polisi wa kawaida, Polisi wa Utawala (AP), Kikosi cha GSU na Kitengo cha Trafiki,” amesema Arum.

“Tunapanga kufungua milango saa 3:00 asubuhi ili mashabiki waburudike na onesho la Musa Jakadala na pia watazame mchezo wa utangulizi kati ya Gor Mahia Queens na AFC Leopards Queens utakaoanza saa 5:30 asubuhi,” amesema Arum.

Wauzaji wa vyakula na vinywaji watalipia Sh500 kabla ya kuingia na bidhaa zao uwanjani. Hata hivyo, wanaouza maji, soda na vileo watalazimika kumimina vinywaji kwenye vikombe vya plastiki wanapowauzia mashabiki.

“Uuzaji wa vinywaji kwenye chupa au makontena ambayo yanaweza kutumika kama silaha hautaruhusiwa. Lazima wauze kwenye vyombo visivyo na madhara,” amesema Arum.