Yanga yatua kwa Makambo

Muktasari:

WAKATI mashabiki wa Yanga wakiendelea kujiuliza mabosi wao wanataka mshambuliaji wa gani ili kumsajili kwa lengo la kuimarisha safu yao ya ushambuliaji, lakini habari mpya ni kwamba straika Heritier Makambo anajiandaa kurudi Jangwani baada ya kuanza mazungumzo ya siri na mabosi hao.

WAKATI mashabiki wa Yanga wakiendelea kujiuliza mabosi wao wanataka mshambuliaji wa gani ili kumsajili kwa lengo la kuimarisha safu yao ya ushambuliaji, lakini habari mpya ni kwamba straika Heritier Makambo anajiandaa kurudi Jangwani baada ya kuanza mazungumzo ya siri na mabosi hao.

Tangu Makambo alitimke klabuni hapo baada ya kuichezea kwa msimu mmoja tu wa 2018-2019, Yanga imekuwa ikitaabika kumpata straika mchana nyavu, kwani mastraika walioletwa Jangwani ili kuziba pengo lake akiwamo, David Molinga na waliopo sasa wameshindwa kufikia kasi yake.

Mkongoman huyo aliondoka akiwa ameifungia Yanga mabao 17 akisaidia timu yake kushika nafasi ya pili nyuma ya Simba, lakini akimaliza nafasi ya tatu ya orodha ya wafungaji wa msimu huo nyuma ya kinara Meddie Kagere wa Simba aliyefunga 23 na Salim Aiyee aliyekuwa Mwadui aliyetupia 18.

Lakini sasa, habari ziwafikie mashabiki wote wa Yanga kwamba jamaa amewekewa mzigo wa maana mezani mwake na huenda akarejea kukinukisha Jangwani.

Uhakika ni kwamba Yanga itasajili mastraika wawili wazuri ukiwa ndio mpango namba moja wa mabosi wa timu hiyo iliyo chini ya Kocha Nasreddin Nabi, na jina la Makambo linaonekana kuzidi kung’aa katika msako wa mabosi hao wa klabu hiyo ambayo usiku wa jana ilikuwa uwanjani kuvaana na Mwadui katika mechi ya Ligi Kuu.

Utamu ni kwamba Makambo ni kama amechoka maisha ya Guinea akiwa na klabu ya AC Horoya iliyomnunua miaka mitatu iliyopita akitokea Yanga na sasa yuko tayari kurejea tena Jangwani kuendelea kuwajaza kama alivyofanya wakati akikiwasha chini ya kocha Mwinyi Zahera.

Yanga inaamini Makambo anaweza kuja kuwasaidia kwa kuwa anajua vyema mazingira na falsafa ya soka lao na kikubwa zaidi wako mabosi wengi wanaona ni bora kuchukuliwa mkongomani huyo kuliko kuja na mtu mpya asiyejua mazingira ya soka la Yanga na hata Tanzania.

“Naona watu wengi hasa viongozi wenzangu wana shauku ya kutaka na kuona Makambo arudishwa na bahati nzuri mwenyewe anaonyesha yuko tayari na anatamani sana hatua hiyo,” alisema mmoja wa vigogo wa Yanga, aliyeongeza kwa kusema; “Unajua hii ni mara ya pili tunataka kukamilisha hii muvi na mara ya kwanza uongozi wa klabu yake uliweka ugumu hasa yule rais wao hatujajua sasa.”

Mwanaspoti inafahamu kwamba msimu uliopita Makambo, alikuwa tayari kurejea Yanga lakini Rais wa Horoya wakati huo ambaye pia ni Rais wa Shirikisho la Soka nchini Guinea, Antonio Souare aligoma kumuachia huku kocha wa wakati huo timu ikifundishwa ma Mfaransa Patrice Neveu.

Horoya ambayo sasa ni mabingwa tena wa Guinea wanataka kuunda upya safu yao ya ushambuliaji na katika hesabu hizo Makambo ambaye hajapata nafasi ya kutosha ya kuanza katika kikosi hicho jina lake limo katika watu ambao wanaweza kuondolewa.

Rais wa sasa wa Horoya, Soufiane Souare ambaye ni mtoto wa Antonio haitakuwa vigumu kwake kumuondoa Makambo kutokana na tayari ameshatangaza kwamba anataka washambuliaji wa maana katika safu yao ya ushambuliaji na eneo la kiungo.


BOXER AKOLEZA

Beki wa kulia wa Yanga, Paul Godfrey ‘Boxer’ aliyecheza kikosi kimoja na Makambo, alisema akija straika huyo watatisha upya.