Yanga wamkataa mwamuzi pambano la Simba

Klabu ya Yanga imeaza kuingiwa na mchecheto kuelekea mechi ya kombe la Shirikisho la Azam (ASFC) dhidi ya Simba, mchezo unaotarajiwa kupigwa Julai 25 katika uwanja wa Lake Tanganyika baada ya kutokuwa na imani na mwamuzi wa pambano hilo Ahmed Arajiga.

Taarifa iliyotolewa na Klabu hiyo kupitia kwa Idara ya Habari na Mawasiliano inasema kuwa "Uongozi wa Klabu ya Yanga SC, umeshtushwa na chaguo la mwamuzi Ahmed Arajiga kwa ajili ya kuchezesha mchezo wa fainali ya kombe la Shirikisho (ASFC) utakaofanyika Kigoma Jumapili Julai 25"

"Hali hiyo imetokana na ukweli kwamba mwamuzi huyo ndiye amehusika katika kuchezesha mechi za wapinzani wetu zilizofuatana katika mashindano haya, katika hatua ya robo fainali, nusu fainali na sasa amepangwa katika fainali"

"Uongozi wa Yanga una amini Tanzania ina waamuzi wengi wenye uwezo hivyo kitendo cha kumrudia mwamuzi mmoja katika mechi tatu za timu moja katika shindano moja kinatia shaka kwetu kama Klabu na mashabiki wetu pia"

"Hivyo basi tunaomba Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na menejimenti ya mashindano haya kutafakari juu ya uamuzi wa kumtumia mwamuzi huyu katika mchezo huo mkubwa wa fainali"


IMEANDIKWA NA DAUDI ELIBAHATI