Manara amjibu tena Barbara

SAA chache baada ya Mtendaji Mkuu wa Simba, Barbara Gonzalez kumjibu Msemaji wa klabu hiyo, Haji Manara baada ya kusambaa sauti mitandaoni, msemaji huyo ameibuka tena na kujibu juu ya sauti hizo.
Manara amedai kuwa hakusambaza sauti hizo zilizokuwa gumzo mtandaoni akimtuhumu Barbara kumfanyia mtimanyongo ndani ya klabu hiyo, jambao ambalo Mtendaji huyo alisema hana muda wa kulijadili kwa sasa kwa vile akili zake zimeelekezwa katika fainali ya ASFC.
Manara ameandika kwenye ukurasa wake wa Instagram akidai hajasambaza sauti hiyo kama watu wanavyodhani na ataliongelea jambo hilo mechi yao dhidi ya Yanga Julai 25 mkoani Kigoma ikiisha.
"Jana nilisema sitaongea tena kuhusu hili jambo hadi game ipite na mamia ya watu wamenirai hivyo pia. Lakini Kwa sababu anazozijua yeye usiku wa jana akaamua kuvujisha clip niliyomtumia yeye WhatsApp!!"
Ameandika kuwa; "Wengine wanadhani mm ndio nimeituma hyo clip, sina muda na hivyo vitu, lau ningetaka kuachia lolote jana , basi ningeachia mambo ya aibu na tuhuma zake zilizojaa vitisho kwangu."
Manara ambaye anafahamika kwa jina la utani Bugati amewataka mashabiki wa timu hiyo kuelekeza fikra zao kwenye mechi ya Jumapili kisha wamsubiri ataongea zaidi.
"Narudia tena na tena sitaki kwa sasa kuongea lolote hadi mechi hii ipite, nisilazimishwe kusema sasa. Yoyote anaedhani vinginevyo asubiri Jumatatu kisha tutoe hukumu. Sitachafuka na ukweli utaniacha huru na mtajua kila kitu. Focus yetu tuipeleke Kigoma tafadhali, nikiyasema sasa Simba ndio itaumia," ameeleza Manara.