Yanga kutambulisha chuma kingine leo

Muktasari:
- Maxi ambaye alikuwa nahodha wa Maniema anahesabika kuwa winga bora wa kulia aliyesalia kwa sasa katika Ligi ya DR Congo, pia na ubora wa kucheza kama kiungo mshambuliaji na kupiga pasi za mabao.
Yanga imesema zoezi la kutambulisha mastaa wao wapya kuelekea msimu ujao litaendelea Leo watakapomtambulisha nyota wao mwingine mpya.
Afisa Habari wa Yanga, Ally Kamwe amesema watatambulisha chuma kingine siku ya leo akitarajiwa kuwa staa wao wa nne kutambulishwa.
Ingawa Kamwe hakuweka hadharani kuwa ni staa yupi ambaye atatambulishwa lakini Mwanaspoti linafahamu mabosi wa Yanga Leo walikuwa kikao cha kumalizia uhamisho wa winga wao mpya Maxi Nzengeli ambaye alitua nchini jana usiku akitokea kwao DR Congo.
Maxi ambaye alikuwa nahodha wa Union Maniema anasifika kuwa winga bora aliyesalia Ligi Kuu ya Congo akiwa na ubora wa kujua kuzalisha pasi za mabao.
Tayari Yanga imeshawatambulisha wachezaji wawili wazawa winga Nickson Kibabage, kiungo Jonas Mkude huku beki Mganda Gift Fred akiwa staa pekee wa kigeni aliyetambulishwa mpaka sasa.
Ujio wa Maxi kama mambo yataenda sawa atakuja kuchukua nafasi ya Mkongomani mwenzake Twisila Kisinda ambaye amerudishwa klabu yake ya RS Berkane ya Morocco baada ya kumaliza kutumikia mkataba wake wa mkopo wa msimu mmoja.