Yanga Dar watofautiana

Muktasari:

SIKU chache kabla ya Yanga kufanya Mkutano Mkuu, baadhi ya wanachama wa klabu hiyo wameanza kutofautiana katika moja ya kipengele kwenye rasimu ya mabadiliko ya katiba yao kuelekea mfumo mpya wa uendeshaji.

SIKU chache kabla ya Yanga kufanya Mkutano Mkuu, baadhi ya wanachama wa klabu hiyo wameanza kutofautiana katika moja ya kipengele kwenye rasimu ya mabadiliko ya katiba yao kuelekea mfumo mpya wa uendeshaji.

Yanga wanatarajiwa kufanya mkutano huo Juni 27, ili kupitisha juu ya mfumo wa uendeshaji wa klabu hiyo kutoka ule wa wanachama uliopo sasa na tayari mabosi wao wamehimiza wanachama kuchangamka kulipia kadi zao.

Hata hivyo, Mwanaspoti ilifanya mahojiano jana na viongozi wa matawi kutoka Ilala, Kinondoni pamoja na Temeke na kujua namna ambavyo wameanza kutoa elimu juu ya mabadiliko yao ya mfumo kabla ya kwenda kuupisha kwenye mkutano huo.

Mwenyekiti wa Matawi ya Ilala, Kais Edwin alisema walikutana wiki iliyopita walipitia rasmu ya katiba yao huku kipengele cha uwakilishi wa wanachama kwenye mkutano mkuu kikipingwa.

“Hapo nyuma ni kila mwanachama ambaye amelipia uwanachama wake anapata nafasi ya kuhudhuria mkutano mkuu, lakini sasa hivi kipengere hicho kinasema kuwa wanachama watano kutoka kila tawi ndio watapata nafasi kitu ambacho kinapingwa,” alisema Kais.

Kwa upande wa Kinondoni kupitia kwa Shaaban Mgonja alisema, kipengere hicho kilionekana kukataliwa huku wanachama wakihitaji kupata uwakilishi wao kama zamani na sio kutuma uwakilishi.

Naye Mwenyekiti wa matawi ya Yanga Temeke, Mohamed Kalambo alisema kwa upande wao kipengele hicho kiliungwa mkono.

“Uwakilishi wa watu wachache walikubali kutokana na idadi kubwa na wanayanga kwa sasa na eneo la kuwaweka wote kwa wakati mmoja, lakini la matawi yasiwe na Kamati lilipingwa.”