TFF yaishushia rungu Azam
Muktasari:
- Kamati ya Mashindano ya TFF iliyokutana jijini Dar es Salaam, ilipitia taarifa ya mchezo huo uliopigwa Julai 4, 2026, kwenye Uwanja wa Gombani kisiwani Pemba na kutoa uamuzi dhidi ya Azam pamoja na baadhi ya wahusika wa benchi la ufundi na wachezaji wake.
SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF), limeshusha rungu zito kwa Azam FC kufuatia matukio yaliyotokea baada ya fainali ya Kombe la Shirikisho la CRDB ilipopoteza kwa bao 1-0 dhidi ya Simba.
Kamati ya Mashindano ya TFF iliyokutana jijini Dar es Salaam, ilipitia taarifa ya mchezo huo uliopigwa Julai 4, 2026, kwenye Uwanja wa Gombani kisiwani Pemba na kutoa uamuzi dhidi ya Azam pamoja na baadhi ya wahusika wa benchi la ufundi na wachezaji wake.
Klabu hiyo imetozwa faini ya Sh50 milioni kwa kosa la kugomea sherehe za kukabidhiwa zawadi ya mshindi wa pili baada ya mchezo huo wa fainali kuisha, adhabu inayohusisha kanuni ya 27:7 ya Ligi Kuu.
Uamuzi huo haukuishia hapo, kocha wa makipa wa Azam, Roudy Mountaro, amefungiwa michezo minne na kutozwa faini ya Sh2 milioni kwa kumshambulia mwamuzi, huku kipa wa timu hiyo, Zuberi Foba naye akifungiwa mechi tatu na faini ya Sh2 milioni kwa kosa hilohilo la kumshambulia mwamuzi baada ya filimbi ya mwisho.
Katika hatua nyingine, Jamal Salum Mohamed ambaye ni kiongozi wa Azam, amepelekwa kamati ya nidhamu ya TFF kutokana na madai ya vitendo vya nidhamu.
Ikumbukwe kuwa, baada ya mchezo huo, Jamal alifanya mkutano na vyombo vya habari akionyesha kutokubaliana na kinachofanywa dhidi ya timu hiyo katika mechi zake mbalimbali akidai inanyimwa haki huku akitoa shutuma mbalimbali kwa mamlaka hiyo ya soka nchini.
Mbali na Jamal, kamati hiyo ya mashindano pia imempeleka katika kamati hiyo, Afisa wa Simba, Ally Shantry maarufu kwa jina la Chico kutokana na madai hayo hayo ya utovu wa nidhamu kwenye mchezo huo.