Tanzania yaaza vizuri Cosafa

MICHUANO ya Cosafa upande wa Wanawake imeendelea leo Jumatano Novemba 4 ambapo timu ya Taifa ya Tanzania chini ya umri wa miaka 17 imeanza vizuri kwa kuwafunga Comoro bao 5-1.
Michuano hiyo ambayo leo ilikuwa ni siku ya pili tangu ianze inafanyika nchini Afrika Kusini ambapo mechi hiyo ilianza saa 7:30 mchana.
Tanzania ilijipatia bao la kwanza dakika ya 20 kupitia mshambuliaji wake Aisha Masaka aliyefunga mabao mawili ambapo bao la pili lilifungwa dakika 59.
Mpira uliendelea kwa kasi huku Tanzania ikionekana kulisakama zaidi lango la wapinzani wao ingawa dakika ya 26, Comoro walipata bao kwa njia ya penalti ambayo ilipigwa na Noussrat Mistoihi.
Timu hizo zilikwenda mapumziko zikiwa sare ya bao 1-1 ingawa baada ya mapumziko hayo mambo yalikuwa magumu kwa wapinzani kwani walijikuta wakifungwa mabao manne.
Bao la pili la Tanzania lililofungwa na Aisha lilitokana na kuunganisha mpira uliotemwa na kipa wa Comoro, Ben Ali Amina.
Dakika ya 71, Joyce Lema aliipatia Tanzania bao la tatu baada ya kupiga shuti kali nje ya boksi la wapinzania wao huku Mwamvua Haruna akiofunga bao la nne dakika ya 82 kabla ya Protasia Mbunda kupigilia msumari wa mwisho dakika ya 88.
Baada ya mchezo huo Tanzania itaumana na Zambia keshokutwa Ijumaa mechi itakayochezwa kuanzia saa 7:30.
Michuano hiyo itachezwa kwa mfumo wa ligi ambapo timu itakayokuwa kinara ndio itatawazwa bingwa, hivyo kwa sasa Tanzania ndiyo inayoongoza ikiwa na pointi tatu.