Stein, Dar City patachimbika BDL

Muktasari:
- Mchezo huo unaosubiriwa kwa hamu na wapenzi wengi wa kikapu utachezwa saa 2:00 usiku, huku Stein Warriors inayoongoza kuwa na wapenzi wengi katika Ligi ya BDL, inakutana na timu ngumu isiyotabirika ya Dar City.
ULE uhondo wa Ligi ya Kikapu Mkoa wa Dar es Salaam (BDL) unaendelea tena leo kwenye Uwanja Donbosco Upanga wakati Stein Warriors na Dar City zitakaposhuka uwanjani kuonyeshana kazi katika mfululizo wa ligi hiyo inayozidi kushika kasi.
Mchezo huo unaosubiriwa kwa hamu na wapenzi wengi wa kikapu utachezwa saa 2:00 usiku, huku Stein Warriors inayoongoza kuwa na wapenzi wengi katika Ligi ya BDL, inakutana na timu ngumu isiyotabirika ya Dar City.
Timu hiyo inajivunia na nyota kama Jonas Mushi, Mwalimu Heri, Evance Davies na Brian Mramba.
Stein Warriors iliyopanda daraja mwaka huu, katika mchezo wa kwanza iliishinda KIUT kwa pointi 70-62, kisha ikaifyatua Savio pointi 93-74 na kuilaza Mgulani JKT kwa pointi 97-46 kabla ya kupoteza mbele ya UDSM Outsiders kwa pointi 69-65.
Wakati timu zinazoshiriki Ligi ya kikapu mkoa wa Dar es Salaam (BDL) zikimaliza kucheza michezo minne, Stein Warriors ndio inayoongoza kwa kufunga pointi 324.
Inafuatiwa na JKT iliyofunga pointi 280, Mchenga Star (279), ABC (271), UDSM-Outsiders (269), KIUT (264) na Dar City (259).
Nyingine ni Pazi (254), Polisi ( 223), Kurasini Heat (220), Srelio (210), Mgulani JKT (200), Vijana “City Bulls” (182), Savio (197) na DB Oratory (174).
Kwa upande wa Dar City inajivunia nyota kama Hasheem Thabeet, Victor Mwoka, Amin Mkosa na Stanley Mtunguja na ilianza michuano kwa kucheza michezo miwili kwa kuifunga Pazi kwa pointi 62-47 kisha kuilaza Srelio pointi 105-32 na baadaye ikaifunga Savio kwa pointi 92-73.
Hivyo leo, inakamilisha mechi ya nne katika ligi hiyo, lakini ikikutana na timu yenye mizuka mingi na inayotoa ushindani uwanjani, kitu kinachofanya pambano hilo la leo kuvuta hisia za wengi wakitaka kujua ni Dar City au Stein itakayoibuka kidedea.
Michezo mingine itakayochezwa leo kwa upande wanawake, City Queens itacheza na Pazi, Reel Dream itaikaribisha Jeshi Stars na wanaume ABC itacheza na Mchenga Stars.