Stars kuanzia makundi Afcon 2023

TIMU ya Taifa Tanzania 'Taifa Stars' imeingia katika hatua ya makundi kwenye fainali za mataifa ya Afrika inayotarajiwa kufanyika 2023 nchini Ivory Coast.
Tanzania na timu zingine 41 (Jumla 42) zitaingia moja kwa moja katika hatua ya makundi huku wakisubiri timu sita kutoka katika raundi ya awali na kuwa timu 48 ambazo zitakuwa katika makundi 12 (A-L).
Stars imepata uhakika wa kuanzia hatua ya makundi baada ya jana kufanyika droo ya raundi ya awali Douala, Cameroon ikisimamiwa na wachezaji wa zamani Emmanuel Amunike (Nigeria) na Rigobert Song (Cameroon) wakisaidiana na mkurugenzi wa mashindano CAF, Samson Adamo.
Droo hiyo ilihusisha timu 12 ambazo zitacheza raundi hiyo ya awali na baada ya hapo zitapatikana wababe sita ambao wataenda kukutana na timu 42 katika hatua ya makundi.
Raundi ya awali itakuwa kwa mfumo wa kucheza nyumbani na ugenini ambayo itaanza kucheza Machi 21 na marudiano Machi 29,2022.
Mechi ambazo zitachezwa ni;
Eritrea vs Botswana
Sao Tome and Principe vs Mauritius
Djibouti vs South Sudan
Seychelles vs Lesotho
Somalia vs Eswatini
Chad vs Gambia