Simba yamwaga mamilioni Mwananyamala
UONGOZI wa klabu ya Simba umetoa Sh10 milioni kwenye Hospitali ya Rufaa Mwananyamala wodi ya mama na mtoto kwaajili ya kusaidia afya ya mama na mtoto.
Simba imetoa kiasi hicho cha fedha ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea kilele cha Simba Day, Septemba 19 kama ambavyo ufanya kila mwaka hutoa kwa jamii yenye uhitaji.
Mtendaji Mkuu wa Klabu, Barbara Gonzalez amesema mwaka huu wameamua kutoa fedha badala ya vitu ili kutoa wigo kwa uongozi wa Hospitali kununua vitu ambavyo vinahitajika kwa haraka.
"Uongozi ndiyo unajua kitu gani kinahitajika kwa haraka na kiasi cha fedha tulichotoa kitasaidia sehemu fulani ingawa tunajua hakitaweza kumaliza kabisa tatizo," amesema Barbara.
Kwa upande wake Katibu wa Hospitali, Lilian Mwanga ameupongeza uongozi wa klabu kwa msaada huku akiutaka uhusiano huo kuendelea na usiishie leo na kwamba fedha hizo zotatumika kama ilivyokusudiwa.
"Kwa niaba ya Uongozi wa Hospitali naipongeza Simba kwa msaada huu, mnaweza kuuona kama ni mdogo lakini kwetu ni mkubwa na tutaenda kuutumia kama ilivyokusudiwa na tunawakaribisha wakati mwingine," amesema Lilian.