Samatta akalia kuti kavu Fenerbahce

MIAMBA ya soka la Uturuki, Fenerbahce imeripotiwa kuwa na mpango wa kumpiga bei mshambuliaji wao na nahodha wa Taifa Stars, Mbwana Samatta ambaye awali alijiunga na timu hiyo kwa mkopo kabla ya kukubaliana kufanya uhamisho wa moja kwa moja.

Samatta, ambaye alitua Villa Park kwa ada ya uhamisho wa Pauni 8.5milion akitokea Ubelgiji ambako alikuwa akiichezea KRC Genk, Januari 2020, alijiunga na Fenerbahce kwa mkopo wa msimu mzima, Septemba mwaka jana.

Akiwa na uzi timu hiyo kwenye mchezo wake wa kwanza kutupia, nahodha huyo wa Taifa Stars aliweka kambani mabao mawili ambapo ilikuwa mwanzoni mwa Oktoba, 2020 na ilikuwa mchezo wa Ligi dhidi ya Fatih Karagumruk. Walishinda kwa mabao 2-1.

Tangu hapo Samatta ameishia kufunga mabao mengine mawili ndani ya michezo 17 aliyocheza ya Ligi ambapo ilikuwa dhidi ya Ankaragucu na Kayserispor.

Kwa mujibu wa chanzo cha uhakika kutoka Uturuki, ambacho kimefichua ukweli wa mambo yalivyo, kimeripoti kuwa Fenerbahce wameanza mipango ya kutaka kumpiga bei mshambuliaji huyo na kutafuta aliyebora zaidi, vinginevyo aongeze makali yake.

Inaelezwa kuwa nahodha huyo wa Taifa Stars hajafikia matarajio ya kocha wa timu hiyo, Erol Bulut aliyokuwa anatarajia kutoka kwake.