Ruvu Shooting yawekwa sokoni

Muktasari:

  • Ruvu ilikuwa timu ya kwanza kushuka daraja msimu uliopita kwa kuburuza mkia ikiwa pamoja na Polisi Tanzania na Mbeya City, baada ya kupanda msimu wa 2017-2018 inadaiwa mabosi wake wameiweka sokoni wakisubiri mtu wa kuinunua ili kuachana nayo jumla.

WAZEE wa Kupapasa, Ruvu Shooting imeshuka daraja kutoka Ligi Kuu Bara na msimu ujao itacheza Ligi ya Championship, huku ikidaiwa ipo kwenye mpango wa kuuzwa.

Ruvu ilikuwa timu ya kwanza kushuka daraja msimu uliopita kwa kuburuza mkia ikiwa pamoja na Polisi Tanzania na Mbeya City, baada ya kupanda msimu wa 2017-2018 inadaiwa mabosi wake wameiweka sokoni wakisubiri mtu wa kuinunua ili kuachana nayo jumla.

Habari ambazo Mwanaspoti imezipata ni kwamba mabosi wa timu hiyo wanataka kuwekeza nguvu zaidi kwenye timu moja iliyopanda Ligi Kuu ya JKT Tanzania, hivyo wanatafuta mtu atakayeweza kuinunua Ruvu.

Chanzo hicho kilisema; "Kuna mpango huo ingawa sidhani kama jambo hili litafanikiwa, kununua timu sio kazi kubwa, kazi ipo kwenye uendeshaji."

Hata hivyo, viongozi wa Ruvu hawajatangaza mchakato wowote wa kuuzwa kwa timu yangu na hata Msemaji wa klabu hiyo,Masau Bwire alipotafutwa na Mwanaspoti jana na kuulizwa juu ya mchkato huo alisema kma upo watautangaza rasmi.

"Kwani mmesikia wapi kuwa tunaiuza timu yetu. Enewei, kukiwa na mpango huo tutatangaza rasmi, " alisema Masau.